Na MWANDISHI WETU
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Asha-Rose Migiro, amesisitiza dhamira ya muda mrefu ya Tanzania katika kuendeleza utawala wa kidemokrasia, ushiriki wa kisiasa kwa njia ya amani na kuheshimu utawala wa sheria.
Dk. Asha-Rose alisema hayo jijini Dodoma, alipozungumza na Balozi Parfait Onanga-Anyanga ambaye ni Mwakilishi Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Umoja wa Afrika na Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa iliyopo Addis Ababa, Ethiopia (UNOAU).
Balozi Onanga-Anyanga yupo nchini Tanzania kwa nafasi yake ya Mjumbe Maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Antonio Guterres.
Kikao hicho ni sehemu ya ushirikiano na mjumbe huyo na wadau wa kitaifa kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu mustakabali wa kisiasa kufuatia uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, mwaka jana pamoja na jitihada za kuimarisha amani, demokrasia na mshikamano wa kitaifa nchini.
Dk. Migiro alisema Tanzania inaendelea kuongozwa na misingi ya Mkataba wa Umoja wa Afrika wa Demokrasia, Uchaguzi na Utawala Bora na viwango vya kimataifa vilivyowekwa katika tamko la kimataifa la Haki za Binadamu na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa.
Alieleza kuhusu mageuzi ya kisheria katika Tume Huru ya Uchaguzi na taasisi nyingine yaliyofanyika kwa lengo la kuimarisha mfumo wa uchaguzi, ikiwemo kutungwa sheria mpya za uchaguzi mwaka 2024 na hatua zilizolenga kuongeza uwazi, uwajibikaji na imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.
Mazungumzo hayo pia yaligusia vurugu zilizojitokeza katika baadhi ya maeneo nchini wakati na baada ya uchaguzi mkuu, ambapo hatua stahiki zilichukuliwa kurejesha utulivu na amani nchini.
Pande zote mbili zilisisitiza umuhimu wa kuendelea mazungumzo na maridhiano miongoni mwa wadau wa kitaifa.
Katibu mkuu huyo wa CCM, alimthibitishia Balozi Onanga-Anyanga kuwa Tanzania itaendeleza uhusiano wake na jumuiya ya kimataifa katika kuimarisha amani, usalama na maendeleo jumuishi.
Aidha, alisema Chama kinapongeza ushirikiano madhubuti uliopo kati ya Tanzania na Umoja wa Mataifa na kuthibitisha dhamira yake ya kustawisha umoja wa kitaifa, utulivu na demokrasia nchini.




