BALTAZAR MASHAKA Na SUPERIUS ERNEST
SERIKALI imesema uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanyika katika sekta ya usafiri na usafirishaji kwa Mkoa wa Mwanza na Kanda ya Ziwa kwa ujumla, utachochea ukuaji uchumi wa Tanzania na nchi za Maziwa Makuu.
Pia, imesema mkoa huo wa kimkakati kwa uwekezaji ukitarajiwa kuwa kitovu cha biashara kwa nchi hizo.
Hayo yalisemwa jijini Mwanza na Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, alipozungumzia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali
Alisema kwa kutambua umuhimu huo wa ukuaji uchumi, mkoa wa Mwanza unachangia sh. trilioni 14.8 katika pato la taifa, sawa na asilimia 7.2 ambapo ni mkoa wa pili ukitanguliwa na Dar es Salaam unaochangia sh. trilioni 17.08.
Msigwa alisema hadi hivi sasa mkoa huo umeshapokea sh. bilioni 405.2 ambazo sawa na asilimia 64 ya bajeti, huku sh. bilioni 77.3 zimeelekezwa katika shughuli za maendeleo.
Akielezea ujenzi wa meli kubwa ya kisasa ya New MV Mwanza ambao umekamilika, Msigwa alisema ni sehemu ya jitihada za serikali kuboresha miundombinu ya usafiri katika Ziwa Victoria na kufungua fursa mpya za kiuchumi kwa sekta ya utalii na biashara.
Msemaji huyo alieleza uwepo wa meli hiyo yenye uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo utaimarisha usafiri wa majini kati ya jiji la Mwanza na nchi jirani zikiwemo Uganda na Kenya.
Kwa mujibu wa Msigwa, hatua hiyo itaongeza mzunguko wa biashara na kukuza shughuli za kiuchumi zinazohusisha bidhaa za pamba, madini, samaki, nyama na maziwa.
Aliwahimiza wafanyabiashara na wadau wa utalii kutumia fursa hiyo kikamilifu, akisisitiza serikali haitaridhika kuona uwekezaji mkubwa kama huo unakosa tija kutokana na uhaba wa abiria au mizigo.
MRADI WA SGR
Katika hatua nyingine, Msigwa alisema serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi wa reli ya kisasa ya kiwango cha kimataifa (SGR), unaogharimu zaidi ya sh. trilioni 31.
Alisema ujenzi wa reli hiyo unaendelea, ambapo kipande cha Makutupora kimefikia asilimia 15, Mwanza-Isaka asilimia 68, Tabora-Isaka asilimia 165 na Tabora-Kigoma asilimia 10.
Alisema lengo la serikali ni kuhakikisha mwaka 2028 reli hiyo inafika Mwanza kurahisisha usafirishaji wa mizigo kwenda nchi jirani kwa ufanisi zaidi.
Msigwa alisema serikali ina mpango wa kujenga reli nyingine ya kisasa inayotumia umeme, yenye uwezo wa kusafirisha tani 10,000 za mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam, tofauti na reli ya sasa ya MGR inayotumia mafuta na kubeba tani 600 hadi 800.
Vilevile, alisema serikali inaendelea na mpango wa kujenga meli nyingine ya mizigo yenye uwezo wa kubeba tani 3,00 katika Ziwa Victoria kwa gharama ya sh. bilioni 145, hatua itakayokuza uchumi na kuimarisha zaidi biashara katika ukanda huo.
Akizungumzia Dira ya Maendeleo ya taifa, Msigwa alisema ifikapo mwaka 2050, Tanzania inalenga kufikia pato la mtu mmoja mmoja la dola za Marekani 7,000, huku sekta binafsi ikitarajiwa kuwa mhimili mkuu wa ukuaji wa uchumi kwa kuchangia takriban trilioni moja.
Alibainisha serikali chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, imejipanga kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inatekelezwa kwa wakati kufungua fursa zaidi za kiuchumi na maendeleo kwa ustawi wa wananchi.
Miradi mingine ya maendeleo iliyotekelezwa mkoani Mwanza ni daraja la Kigongo-Busisi, ambalo linaendelea kirahisisha maisha ya wananchi na kuchochea ukuaji uchumi.
Daraja hilo limekuwa nyenzo kubwa ya ukuaji uchumi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa hususan katika kusafirisha mizigo mingine kwenda nje ya nchi.
“Pia, hapa Mwanza tunao mradi wa vizimba vya samaki serikali ikiwa imewekeza sh. bilioni 8.9 kusaidia vijana kupata nyenzo za uvuvi, kuwezesha ufugaji wa samaki kupitia vikundi mbalimbali,”alisema Msigwa.
Kadhalika, alisema serikali inaendelea kujenga soko kuu la mjini linalogharimu sh. bilioni 26.6 likiwa la kisasa na kukuza ajira. Lengo kuwa Kariakoo ya Kanda ya Ziwa na kutumika kimkakati.
Msigwa aliongeza ujenzi wa daraja Simiyu ambalo mkataba wake wa usanifu sh. bilioni 48.8, umefikia asilimia 67 ya utekelezaji, huku upanuzi uwanja wa ndege ukigharimu sh. bilioni 29.3 na mchakato wa kuanza ujenzi wa terminal ya kisasa kuwa na uwanja mkubwa zaidi ukiendelea.




