Na Ramadhani Semtawa
MWENYEKITI wa Tume ya Kuchunguza Matukio ya Oktoba 29, Jaji Mkuu mstaafu, Mohamed Chande, amejibu hoja tisa nzito, huku akiwataka Watanzania kutumia muda wa nyongeza kutoa ushahidi zaidi, kwa kuwa anatambua matumaini yao makubwa na jumuiya ya kimataifa kwa Tume hiyo ambayo ni huru, haina dalali wala kuamrishwa.
Jaji Chande alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam, alipoeleza sababu nne za Tume kuomba muda wa nyongeza, akianisha moja ni kuendelea kupokea na kuchambua ushahidi kisayansi hivyo, kuwataka Watanzania zaidi kuwa huru kujitokeza.
Katika mkutano huo, ambao alipokea maswali mbalimbali na kujibu kwa kina, Jaji Chande alisema anajua matumaini makubwa ya watu kuhusu Tume na aliwahikikishia iko huru wala haina dalali.
USHAHIDI
Alifafanua, kazi za Tume zinaongozwa na ushahidi uliowasilishwa ambao katika siku za mwisho kabla ya kuongezewa muda wa ziada, Watanzania zaidi wamekuwa wakiutoa hivyo kuamua kuchukua.
Kwa mujibu wa Jaji Chande, watu ambao wana ushahidi, lakini hawauwasilishi hautafanyiwa kazi, kwa kuwa Tume inafanyia kazi ushahidi uliowasilishwa mbele yake.
“Kazi ya Tume inaongozwa na ushahidi. Mtiririko wa ushahidi ni mkubwa. Ndiyo maana tumeomba muda hatuwezi kuacha ushahidi uliotufikia. Tunaamini muda tulioomba utatosha. Wengine wenye ushahidi tunawakaribisha. Sisi hatulazimishi watu kwa amri bali hiari katika kutoa ushahidi,”alifafanua Jaji Chande.
SABABU ZA TUME KUONGEZEWA
Jaji Chande alizitaja nne; kuwa ni uzito, ukubwa, kina cha kazi na kuendelea kupokea ushahidi ambao unachambuliwa kisayansi kujua uhalisia wake.
Alitoa mfano, zipo picha zilizopigwa kwa satelite na kusambazwa mitandaoni hivyo, kuhitaji uchambuzi wa kisayansi kutoka kwa wataalamu kubaini uhalisia wake.
“Zipo sababu nne; kwanza kupata ushauri wa kitaalamu. Kuna picha zilipigwa kwa satelite, lazima wataalamu wetu wazipitie. Watatushauri na sisi tutapima. Pili, kuchambua ushahidi. Watu wanaendelea kuleta ushahidi, tunataka tuwafikie wengi zaidi.
Jumuiya ya kimataifa ina matumaini makubwa na ripoti hii. Watanzania wana matumaini makubwa pia. Hivyo tumeona ni muhimu itafsiriwe kwa Kiswahili na Kingereza na tufanye majumuisho,” alifafanua akionesha uzito, kina, ukubwa na haja ya kuendelea kupokea ushahidi.
MATARAJIO RIPOTI TUME
Jaji Chande alisema Tume inaamini ripoti itakayotoka itawafanya waathirika wa ghasia za Oktoba 29, kujihisi wametendewa haki kwa kiasi kikubwa.
“Tunataka ripoti ikitoka waathirika wa matukio ya Oktoba 29 wajione wamo ndani ya ripoti. Tunataka baada ya matokeo ya Tume twende mbele kama taifa,” alifafanua Jaji Chande.
Alifafanua Watanzania na jumuiya ya kimataifa wana matumaini makubwa na matokeo ya Tume, hivyo wana deni kuhakikisha wanafanya kazi hiyo kwa weledi bila kuacha ushahidi.
UHURU WA TUME
Kuhusu uhuru wa Tume, alisema ni huru kwa asili kuanzia sheria iliyoianzisha, viapo vya wajumbe na hakuna mtu anayewaamrisha chakufanya.
Jaji Chande alifichua Tume anayoiongoza ina watu makini, ambao wanajua jambo lililotokea Oktoba 29 ni kubwa linalohitaji weledi katika kushughulikia.
Aliongeza baada ya kupewa hadidu za rejea Tume hiyo iliweka kanuni zake yenyewe akisisitiza: “Uhuru wetu ulianza baada ya kupokea hadidu za rejea. Tuliandaa kanuni zetu. Tuliamua ushihidi uwe ni hiari kwa mtu kuutoa.”
Katika kuonesha Tanzania iliwahi kuwa na Tume mbalimbali huru, alisema ilikuwepo ya Jaji Musa Kipenka, iliyochunguza mauaji ya wafanyabiashara wa madini wa Mahenge huku yeye akiongoza Tume ya sakata la Ihefu.
Mwanasheria huyo mwenye hadhi kubwa kimataifa, alifafanua tofauti na Tume mbalimbali za kimataifa ambazo ameongoza; Tume ya ghasia za Oktoba 29 inapata ushirikiano mkubwa kutoka serikalini na wadau mbambali.
“Zipo Tume hata mazingira ya kufanyia kazi ni magumu. Kwa mfano, Sudan haitambui Tume ya Umoja wa Mataifa Kuchunguza ukiukwaji wa haki za binadamu (Mji wa el Fasher), hapa kwetu ni tofauti. Tunapata ushirikiano mkubwa,”alifafanua.
Alisema Tume hiyo ya nchini itakayofanya kazi kwa siku 153, hutumika katika nchi za Jumuiya ya Madola, akitoa mfano Canada imewahi kuwa nazo takribani 500 ikiwemo ya uchunguzi wa damu kuchanganyika na watu kuambukiwa HIV na TB, Tanzania iliunda kati ya sita hadi saba na Afrika Kusini 25.
UKOMO WA TUME
Kuhusu kama Tume itamaliza kazi Aprili 24 na kutoongezewa tena muda, alijibu ndilo lengo kwa kuwa safari imefikia ukingoni.
Alifafanua kazi kubwa iliyobaki ni kuendelea kupokea na kuchambua ushahidi wa mwisho, uandishi wa ripoti kwa lugha ya Kiswahili na Kingereza na kusisitiza; wanatambua kina, ukubwa, uzito na umuhimu wa kazi hiyo.
Jaji Chande alisisitiza, “Tuko karibu mno na mwisho wa safari. Tulianza bila wafanyakazi sasa tunakaribia mwisho wa safari.”
APINGA UPOTOSHAJI
Kuhusu madai Tume imeomba kuongezewa muda kwa malengo ya kuandika ripoti kwa malengo tofauti, alisema:
“Siyo kweli. Sisi ndiyo maripota, maedita, machifu sabu, machifu edita na wamiliki. Hakuna mtu wa kuhaririri chochote zaidi yetu.”
Jaji Chande alisema upotoshaji kuhusu Tume ulianza tangu mwanzo kwa baadhi ya watu kutisha watoa ushahidi kuwa watatekwa, akasisitiza: “Upotoshaji wa aina hiyo unaumiza jamii. Tume inajitegemea asilimia 100. Watu wengi walitoa ushahidi kwa uhuru. Nikitaja idadi ya waliotoa ushahidi mtashangaa.”
USHIRIKI WA GEN Z
Alifafanua Tume ilipokea maoni ya makundi mbalimbali, likiwemo kundi la vijana maarufu Gen Z, bodaboda, wamachinga, mamalishe na mengine kupitia jumuiya zao.
Kuhusu Gen Z, alisema walikutana nao katika ngazi mbalimbali ikiwemo kupitia Shirikisho la Wanafunzi wa Vyuo Vikuu (TAHLISO).
“Wanafunzi wa vyuo vikuu wana serikali yao ya TAHLISO na mabunge yao. Tulikutana nao. Tena tuliwaambia waendeshe wenyewe mijadala, sisi tulikuwa wasikilizaji tu. Walitoa maelezo mazuri tu,” aliongeza.
MARIDHIANO
Jaji Chande alisema, awali Tume ilipaswa kutembelea mikoa sita iliyoathiriwa zaidi na ghasia, hata hivyo baadaye ilitembelea mikoa 11 na wilaya 22 kujifunza maeneo yaliyoathiriwa na ambayo hayakuathiriwa.
Alitoa mfano, katika safari ya Tume kusikiliza wananchi ilikwenda Kilimanjaro na Zanzibar, ambako hakukuwa na madhara ya ghasia za Oktoba 29.
“Tulikwenda Zanzibar kwa sababu hakukuwa na vurugu. Kikubwa wenzetu wana uzoefu wa maridhiano. Mwisho wa siku tutapendekeza maridhiano, ndiyo maana tulienda kujifunza Zanzibar kutokana na uzoefu wao,” alifafanua.
Aliongeza, kwa kutoa mfano mwingine kwenda katika maeneo ambayo hayakuwa na vurugu akirejea Mkoa wa Kilimanjaro ambao haukukumbwa na matukio hayo licha ya kuwa jirani na Arusha na Zanzibar, licha ya kuwa karibu na Dar es Salaam.
KUUNDWA TUME
Tume ya Jaji Chande iliundwa na Rais Dk. Samia, Novemba mwaka jana, baadaye iliongezewa muda hivyo kupaswa kuwasilisha ripoti Aprili 3 na hivi sasa imeongezewa siku 21 hadi Aprili 24.




