Na NASRA KITANA
TIMU za soka za Simba na Coastal Union zinatarajiwa kupambana leo katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Pambano hilo, limepangwa kufanyika leo katika Uwanja wa Mkwakwani, Tanga kuanzia saa 12:30 jioni.
Kuelekea mchezo huo, kocha wa Simba, Steve Barker alisema kila mchezo kwao ni kama fainali, hivyo wamejipanga kupata alama tatu muhimu.
“Unajua tunaelekea mwishoni mwa msimu, hatukubali kuona tunapoteza mchezo wowote ule kwani ushindi ni muhimu.
“Tunamuheshimu mpinzani na tunaingia katika mchezo wetu kuonyesha kiwango kizuri, kulingana na maandalizi mazuri yaliofanyika kwa wachezaji wangu, naamini tunakwenda kupata ushindi katika mchezo huu,” alisema Barker.
Kocha huyo alisema amefanyia kazi kasoro zote zilizojitokeza katika michezo iliyopita.
Nyota wa timu hiyo, David Kameta alisema kama wachezaji wamejipanga vizuri kuhakikisha wanapata ushindi katika mchezo huo muhimu.
“Baada ya mchezo uliopita wachezaji wote tumefanya maandalizi mazuri na kila mmoja yupo tayari kuhakikisha tunapambana kusaka pointi tatu,” alisema Kameta.
Kocha wa Coastal Union Fikiri Elias, alisema timu yake imejipanga vizuri kuhakikisha inashinda mchezo huo, wakiwa uwanja wao wa nyumbani.
“Hatutaki kuwa daraja la kumnyanyua yoyote lazima tutafute alama tatu kwa ajili ya timu yetu na kujiweka nafasi nzuri zaidi,” alisema Elias.
Kocha huyo alisema kila mchezo una ladha yake na wamejiandaa vizuri kucheza dakika 90 kwa kumpa heshima mpinzani wao.
Nahodha wa timu hiyo, Geofrey Manyasi alisema kama wachezaji wamejipanga vizuri kuhakikisha wanashinda pambano hilo.
Katika msimamo wa Ligi, Simba inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi 52 huku Coastal Union ikishika nafasi ya 11, ina alama 25 baada ya timu zote mbili kushuka dimbani mara 23.




