Na AMINA KASHEBA
UONGOZI wa Chama cha Netiboli Mkoa wa Dar es Salaam umesema utakuwa mabalozi wakubwa katika kulinda amani ya nchi kwani ni tunu muhimu.
Akizungumza Dar es Salaam, Mwenyekiti wa chama hicho, Enelisa Chekwaze alisema serikali imehakikisha amani ya nchi inakuwa shwari hivyo ni wajibu wa watanzania kulinda tunu hiyo.
Alisema nchi ikiwa haina amani hakuna jambo lolote linafanyika kwa sababu kunakuwa na vurugu ambazo zinaleta madhara kwa jamii.
“Amani ndiyo kila kitu katika nchi yetu, pia nina imani na tume huru iliyoundwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa sababu watu aliowachagua watafanya kazi kwa weledi,” alisema.
Mwenyekiti huyo alitoa wito kwa watanzania kuhakikisha walinda amani ya nchi kwani ndiyo kitu muhimu ambacho baadhi ya nchi zinashindwa kutokana na vurugu.
“Nchi yetu imekuwa nzuri na baadhi ya watu wanaipenda yote kutokana na amani na upendo uliopo, hivyo ni vyema kuendelea hii hali ili kulinda msingi wetu uliojengwa na Baba wa taifa hayati mwalimu Julius Nyerere,” alisema.




