Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema serikali inatambua na kuthamini mchango wa wafanyakazi wa sekta ya umma na binafsi, katika kukuza uchumi na maendeleo ya taifa.
Dk. Mwigulu alisema hayo jijini Dodoma, katika hafla ya maandalizi ya Mei mosi, mwaka huu, ambayo kitaifa inafanyika mkoani Njombe.
Alisema serikali inaendelea kuwaenzi wafanyakazi nchini kutokana na umuhimu wao mkubwa kwa taifa.
Katika hafla hiyo ya awali, sh. bilioni 1.105 zilikusanywa ambapo Dk. Mwigulu alisema fedha hizo zitasaidia mkoa mwenyeji kukamilisha shughuli za maandalizi ya tukio hilo.
Pia,Waziri Mkuu alilipongeza Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (TUCTA) kwa ubunifu wa kuhakikisha maadhimisho ya Mei Mosi yanaacha alama katika mkoa mwenyeji.
“Wenzetu TUCTA wamekuja na ubunifu kwamba shughuli za Mei Mosi zinaacha alama katika mkoa husika kwa kutekeleza miradi mbalimbali kama walivyofanya katika maadhimisho ya mwaka 2025 mkoani Singida kwa kujenga uwanja wa Bombadia mkoani humo.
“Uwanja ambao sasa umekuwa na manufaa makubwa kwa Wanasingida na Njombe nako wamejiandaa kuacha alama kubwa,”alisema.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Uhusiano, Deus Sangu, alisema maandalizi ya maonesho ya Mei Mosi, mwaka huu, yanaendelea vizuri akisisitiza kuwa kwa siku zilizosalia, maandalizi yote yatakamilika ndani ya wakati.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, alisema maadhimisho hayo ni fursa kwa mikoa yote ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kwa kuwa ugeni wa watu wasiopungua 5, 000 unatarajiwa kushiriki sherehe za Mei Mosi Kitaifa mkoani humo.
Naye, Rais wa TUCTA, Tumaini Nyamhokya, alishukuru na kupongeza kuimarika ushirikiano kati ya serikali na vyama vya wafanyakazi, akisema ushirikiano huo umechangia kuwepo kwa utulivu miongoni mwa wafanyakazi nchini.



