Na SYLVIA SEBASTIAN
MAHAKAMA ya Mwanzo Kariakoo, Dar es Salaam, imemhukumu muosha magari John Mpali, kifungo cha nje cha miezi miwili kwa kufanya usafi mahakama hapo.
Pia, mahakama imemwamuru Mpali kumrudishia sh.110,000 mlalamikaji Mohamed Ango, baada ya kukiri kosa la wizi wa fedha hizo, zilizokuwa ndani ya gari.ed Ango.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Mpoki Mwabela, baada ya mshitakiwa kusomewa shtaka na kukiri.
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mpoki alisema kwa sababu mshitakiwa alikiri shtaka na hakutaka kuisumbua mahakama, hivyo anamhukumu kifungo cha nje cha miezi miwili na kurudisha fedha ifikapo Mei 13, mwaka huu.
Kabla ya kutolewa adhabu, mshitakiwa aliomba mahakama impunguzie adhabu kwa madai ni kosa lake la kwanza na yuko tayari kumrudishia mlalamikaji fedha zake.
Kwa mujibu wa hati ya mashitaka, mshitakiwa alitenda kosa hilo, Aprili Mosi, mwaka huu, Posta karibu na Hoteli ya Holiday Inn, mtaa wa Azikiwe, Dar es Salaam.
Mshitakiwa aliiba fedha zilizokuwa ndani ya gari alilopewa na mlalamikaji kuosha.




