Na MWANDISHI WETU,Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameutembelea mradi wa Mji wa AFCON Fumba uliopo Mkoa wa Mjini Magharibi.
Dk, Mwinyi alifanya ziara hiyo jana, akiambatana na Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk. Riziki Pembe Juma, pamoja na wadau wa mradi wa AFCON Fumba Zanzibar.
Katika ziara hiyo, Rais Dkt. Mwinyi alikagua maeneo mbalimbali ya uwanja huo wa kisasa wa AFCON unaojengwa na kampuni ya ORKUN GROUP ya Uturuki.
Uwanja huo, unatarajiwa kutumika kwa michuano ya AFCON mwaka 2027 itakayofanyika kwa ushirikiano wa nchi tatu za Afrika Mashariki za Kenya, Uganda na Tanzania.
Aidha, Rais Mwinyi alitembelea na kukagua miundombinu inayotarajiwa kujengwa kuzunguka uwanja huo.
Miundombinu hiyo ni hospitali, barabara, migahawa, maduka makubwa (mall) pamoja na huduma nyingine muhimu zitakazouzunguka mji huo wa kisasa.
Uwanja huo, unakadiriwa kuchukua watazamaji 35,000 ukiwa na viwango vya ubora vinavyokubalika na Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF).






