Na MWANDISHI MAALUMU, Dodoma
WANANCHI wameaswa kuchangamkia fursa zinazopatikana katika biashara ya kaboni kwa kuanzisha miradi mbalimbali kulingana na jiografia ya eneo husika na kuacha dhana ya upandaji miti na misitu ndiko inakopatikana biashara hiyo.
Hayo yalisemwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Dk. Richard Muyungi wakati akifungua kikao cha makatibu tawala wa mikoa na wakurugenzi wa halmashauri kuhusu
Programu ya Mageuzi ya Kimkakati ya Mazingira Endelevu Tanzania, kilichofanyika Dodoma, jana, akieleza kuna fursa katika program hiyo ikiwemo biashara ya kaboni.
Alisema fursa ya biashara ya kaboni haipo pekee katika upandaji miti kama ambavyo wengi wanadhani, bali katika nishati safi ya kupikia, miradi ya taka, usafishaji wa miji, taka ngumu na nyingine zote zinazoweza kuwa fursa katika biashara hiyo.
“Ili tuwe na mchango mkubwa kwenye Dira 2050 tunatakiwa kuwa na mpango maalumu na hatutakuwa tukiangalia katika upandaji miti pekee, bali tutaangali pia kwenye nishati safi ya kupikia kuwafikia wananchi,” alisema.
Aliongeza kutokana na heshima ambayo mazingira yamepewa na kuwekwa kwenye Dira 2050 ni vyema sekta ya mazingira nayo ibadilike mchango wake uonekane kwa kuyasimamia mazingira vizuri.
Awali, Naibu Katibu Mkuu (Mazingira), Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda alisema programu hiyo inalenga kuchagiza matokeo makubwa na ya haraka katika kurejesha uoto wa asili, ustawi wa mifumo ikolojia na kuimarisha huduma za kiikolojia ambazo zinachangia katika sekta za uzalishaji nchini.
“Programu hii itatekelezwa Tanzania Bara na Zanzibar kwa kuongeza eneo lenye uoto wa kijani kupitia upandaji miti kwa wingi na usimamizi wa mazingira. Pia, kupunguza uharibifu wa ardhi na ardhi-oevu, kurejesha ardhi na misitu iliyoharibiwa na kukijanisha miji yetu.
“Jitihada hizi zitachangia kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa; kurejesha hekta milioni tano za ardhi, misitu, ardhi-oevu na nyanda za malisho zilizoharibiwa, kuhamasisha usafi wa mazingira na uchumi rejeshi katika usimamizi wa taka.
Aliongeza maeneo ya kimkakati ya utekelezaji wa programu ya mageuzi ya kukijanisha Tanzania ni upandaji miti katika mkoa ya Tabora, Mwanza, Shinyanga, Kigoma, Geita, Singida, Simiyu, Manyara, Kilimanjaro, Arusha, Dodoma, Rukwa na Zanzibar.
Shughuli nyingine ni pamoja na uanzishwaji bustani za kijani katika maeneo ya miji; utunzaji na urejeshaji wa maeneo oevu ya Ziwa Natron, Bonde la Mto Mara, Bonde la Mto Malagarasi Myovosi na Bonde la Mto Kilombero, kudhibiti viumbe vamizi katika maeneo ya mikoa ya Dodoma, Arusha, Mara, Mwanza na Manyara; usafi wa mazingira na urejelezaji wa taka ngumu.
Aidha, Mkurugenzi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais, Kemilembe Mutasa, alisema katika utekelezaji wake, pogramu hiyo muhimu itaweka mkazo katika hatua za kimkakati ikiwemo kukuza uelewa wa umma kuhusu masuala ya hifadhi na usimamizi wa mazingira, kuhamasisha ushiriki wa wadau katika ngazi zote hususan mamlaka za serikali za mitaa na kuweka mfumo wa ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji.





