Na NJUMAI NGOTA
MGOMBEA Mwenza wa Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, amesema wakazi wa maeneo ya Sinza, Ubungo, Makurumla, Kimara na Mabibo jijini Dar es Salaam, wataondokana na tatizo la upatikanaji majisafi na salama.
Hiyo, inatokana na kuimarisha miradi ya maji, kama sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa miaka mitano ijayo.
Balozi Dk. Nchimbi, alisema hayo Viwanja vya EPZA, Mabibo Hosteli, Dar es Salaam, alipowahutubia mamia ya wananchi katika mkutano wa kampeni wa Chama, kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu.
Alisema Ilani ya CCM, imeainisha mikakati madhubuti ya kumaliza kero ya maji, inayowakabili wakazi wa maeneo hayo kwa kuboresha vyanzo vya maji na kuimarisha miundombinu ya usambazaji wake.
“Mbunge wenu wa Ubungo, Profesa Kitilla Mkumbo, amenidokeza kuhusu shida ya maji inayowakabili wananchi wa jimbo hili.
“Ninatambua kero hiyo, niwahakikishie kuwa, Ilani ya CCM imeweka mkazo wa kipekee katika kutatua changamoto hii, kupitia uboreshaji wa vyanzo na miradi ya maji katika maeneo ya Kimara, Mabibo, Sinza, Ubungo na Makurumla,” alisema.
Alisema iwapo watapewa ridhaa ya kuongoza nchi, wataongeza ufanisi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), kwa kuimarisha mifumo ya mawasiliano, kuwawezesha wananchi kutoa taarifa za matatizo ya maji haraka na ufanisi zaidi.
MASOKO YA KISASA NAHUDUMA BORA
Katika kuhakikisha wananchi wa Ubungo wanapata huduma karibu na makazi yao, Balozi Dk. Nchimbi, alisema wamedhamiria kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa masoko ya kisasa 13 ndani ya Wilaya ya Ubungo.
Alisema hatua hiyo, itapunguza adha ya wananchi kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo.
“Nimeelezwa kuwa, wakazi wa Ubungo hulazimika kwenda Mlimani City au Kituo cha Kimataifa cha Afrika Mashariki kununua bidhaa.
“Hili tunaliona na tunalifanyia kazi. Katika miaka mitano ijayo, tutajenga masoko ya kisasa 13 katika wilaya hii, huduma zote zipatikane karibu,” alisema.
UBORESHAJI HUDUMA ZA AFYA
Alisema serikali ijayo ya CCM, itaendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Ubungo, kufanya ukarabati mkubwa katika Hospitali ya Manispaa ya Ubungo kwa kuongeza majengo, vifaatiba na idadi ya watumishi, itoe kutoa huduma za upasuaji wa dharura na matibabu ya magonjwa yote.
Pia, alisema wamekusudia kujenga zahanati tatu na kituo cha afya katika maeneo yenye uhitaji mkubwa, kupunguza msongamano wa wagonjwa na kuimarisha upatikanaji wa huduma.
MIKOPO ASILIMIA 10
Alisema wamedhamiria kuongeza kasi ya utoaji mikopo ya asilimia 10 kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, kupitia halmashauri huku akisisitiza kuwa, mfumo huo, utaboreshwa na kuondoa upendeleo.
Hivyo, aliahidi kuwekwa utaratibu wa kurasimisha biashara za wajasiriamali wadogo, kutambuliwa rasmi na kupata mikopo, elimu ya biashara na fursa nyingine za kiuchumi.
MIPANGO MIJI, MAZINGIRA SAFI
Kuhusu mpango wa makazi na mazingira, Dk. Nchimbi, alisema serikali ijayo ya CCM, itasimamia kikamilifu sheria za mipango miji, kuboresha makazi, kupanga miji kwa ramani rasmi na kuhakikisha mfumo wa ukusanyaji taka, unafanya kazi kwa ufanisi huku wananchi wakihusishwa katika utunzaji wa mazingira.
“Lazima miji yetu ipangwe vizuri. Hili tutalisimamia kwa nguvu zote kwa kuhakikisha kila eneo, lina ramani, makazi bora na mazingira safi,” alisema.
UFANISI WA SERIKALI YA AWAMU YA SITA
Akielezea mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia, alisema yamejikita katika kusimamia uchumi, kupunguza mfumuko wa bei na kuongeza kasi ya ukuaji wa pato la taifa.
“Agosti, mwaka huu, mfumuko wa bei, ulikuwa asilimia 3.1, ukilinganisha na Malawi ambako mfumuko ulifikia asilimia 28.
“Hii ni dalili ya usimamizi mzuri wa uchumi. Kwa miaka minne, uchumi wa Tanzania, ulikua kwa asilimia 4.8, hivi sasa umepanda hadi asilimia 5.6,” alisema.
Alisema hatua za Rais Samia katika kuimarisha diplomasia ya uchumi, zimewezesha Tanzania kuvutia wawekezaji wengi na kuongeza kiwango cha bidhaa zinazouzwa nje ya nchi hasa Kenya.
“Hivi sasa tunauza bidhaa nyingi zaidi nje ya nchi na kiwango cha utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara kimeongezeka. Haya ni mafanikio ya kazi kubwa ya Rais wetu,” alisema.
MBOMBEA UBUNGE UBUNGO
Naye, Mgombea Ubunge wa Jimbo la Ubungo, Profesa Kitilla Mkumbo, alianisha mafanikio mengi yaliyopatikana jimboni humo ukiwemo ujenzi wa barabara.
Pia, Mkumbo alimwombea kura Dk. Samia, wabunge na madiwani wanaotokana na Chama kwa wananchi, katika Uchaguzi Mkuu ujao.




