Na SIMON NYALOBI
ALIYEKUWA Mgombea Urais wa Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), Salum Mwalimu, amesema Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, mwaka jana, ina umuhimu mkubwa katika kujenga mustakabali wa maridhiano ya kitaifa na huku akisifia weledi, ubobevu na uzoefu wa wajumbe wa tume hiyo.
Akizungumza Dar es Salaam, Mwalimu aliwataka wananchi kuelewa umuhimu wa tume na wajumbe wa tume hiyo, kwa kuwa wana sifa stahiki kutekeleza majukumu hayo.
“Hii tume ina umuhimu mkubwa sana kwa wananchi, kwa sababu wananchi watatamani kujua kilichotokea waliohusika wanawajibikaje eeh na kadhalika…, pia wananchi wanatamani kuona kabisa tukio lile halitokei tena katika nchi yetu.
“Kwa hiyo ni tume ya wananchi kimsingi, inaitwa Tume ya Rais, kwa sababu imeundwa na rais kwa niaba ya mamlaka aliyopewa na wananchi, ila ukweli ni tume ya wananchi wenyewe,” alisema.
Akizungumzia umuhimu wa tume hiyo, alisema matokeo yake yatayagusa maisha yao moja kwa moja na itawafikisha wananchi katika maridhiano.
“Matokeo ya tume hii yatawagusa maisha yao moja kwa moja kama ambavyo yaliyotokea Oktoba 29, yaliwagusa na wengine yakawaathiri moja kwa moja, kwa hiyo ‘there is no doubt’, tume itatufikisha kwenye maridhiano.
“Kwa sababu mwisho wa jambo hili lazima Watanzania tuzungumze, hakuna namna nyingine na mwisho wa mazungumzo ni maridhiano,” alisema.
Mwalimu alisema katika maridhiano ni kukiri kwa makosa kwa kuombana radhi, fidia na kukubalina kama taifa kulaani vitendo vya aina hiyo visitoke tena katika taifa.
UAMINIFU NA WELEDI
Kuhusu uaminifu na weledi wa wajumbe wa tume hiyo, alisema wajumbe hao wamesheheni sifa lukuki za kutekeleza jukumu hilo wakiongozwa na Mwenyekiti wao Jaji Mkuu mstaafu Othman Chande, ambaye anaaminika kimataifa.
Mwalimu aliwashangaa wanaohoji weledi wa Jaji Mkuu mstaafu Chande katika kutekeleza jukumu hilo.
“Nani anayeweza kuuliza uaminifu wa mheshimiwa Jaji Chande, unawezaje kuhoji, unaweza kuja na kuhoji uwezo wake, huyu mtu ameshafanya kazi mahakama za ndani, ameshafanya mahakama za kimataifa kimataifa.
“Inawezekana ni yale mambo ya nabii havumi kwao, hivi nchi gani ingepata tatizo lile lisingemchukua Jaji Chande kuwa mwenyekiti wa hiyo tume anakosa nini…, hata huyo mwingine ambaye angeletwa ingewezekana angekuwa kama Jaji Chande au pengine sifa zake zisingekuwa toshelevu kumzidi Jaji Chande,” alisema.
Alifafanua, sifa za mjumbe wa tume hiyo Inspekta wa Jeshi la Polisi mstaafu (IGP) Said Mwema, kuwa aliacha alama katika jeshi hilo kulifanyia mabadiliko, uadilifu na umakini.
Mwalimu alisema alitumikia taifa kwa uadilifu na kujenga heshima katika jeshi hilo enzi zake akiwa madarakani.
Aidha, alisema mjumbe wa tume hiyo Balozi Ombeni Sefue, ni ofisa mwandamizi wa serikali aliyeitumikia serikali kwa muda mrefu.
Pia, alisema mjumbe mwingine wa tume hiyo, Dk. Stergomena Tax, ana sifa ya kuwepo katika tume hiyo kutokana na utumishi wake katika taasisi mbalimbali za ndani na kimataifa.



