Na AMINA KASHEBA
MWANDAAJI wa mashindano ya ‘Miss World Tanzania’, Mustafa Hassan Hassanali amesema uwepo wa utulivu na amani nchini ndiyo sababu ya Tanzania kupata nadasi ya kuwa wenyeji wa mashindano ‘Miss World’.
Hassan alisema hayo Dar es Salaam, kuwa kitendo cha kuwepo amani na utulivu kimewavutia waandaji kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa kuandaa mashindano hayo makubwa duniani.
Hassan ambaye ni mbunifu wa mavazi amewataka Watanzania kutumia fursa hiyo, kujitangaza katika mashindano ya ‘Miss World’ yatakayofanyika mwakani na kushirikisha nchi zaidi ya 130.
“Serikali yetu imetupa fursa ambayo tunapaswa kuichangamkia, kwangu nimeona ni jambo la fahari kuona Tanzania tunakwenda kuwa wenyeji wa mashindano ya ‘Miss World’.
“Haya ni mashindano makubwa hivyo tunapaswa kuipoingeza serikali yetu kwani mwakani tutakuwa na wageni wengi kutoka mataifa mbalimbali,” alisema Hassanali.
Muandaaji huyo aliongeza kuwa kila mtu anapaswa kujipanga na kufanya ambayo litawafurahisha wageni ambao watakuja nchini na kuweka historia.
“Tunaishukuru serikali yetu nchini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha mashindano ya ‘Miss World’ kufanyika hapa nchini, tunapaswa tumsapoti Rais wetu,” alisema.




