Na MWANDISHI WETU
KATIBU Tawala Mkoa wa Mwanza, Balandya Elikana, amesema ajenda ya utunzaji na uhifadhi wa mazingira ni eneo la kipaumbele katika mipango ya maendeleo ya mkoa huo.
Elikana alisema hayo wakati wa mazungumzo baina yake na watalaamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais waliofika mkoani humo kupokea taarifa ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku Mazingira Duniani mwaka huu.
Elikana alisema mkoa wa Mwanza umekuwa mstari wa mbele kuhamasisha juhudi za serikali katika masuala ya utunzaji na usimamizi wa mazingira kwa kuhimiza jamii umuhimu wa uhifadhi mazingira, ikiwemo upandaji miti na shughuli za usafi.
Alieleza kwa kuzingatia umuhimu wa mazingira, sekretarieti ya mkoa huo kwa kushirikiana na halmashauri za wilaya, zinatarajia kuandaa utaratibu wa kuhamasisha vijana kushiriki katika shughuli za utunzaji na uhifadhi misitu.
“Mwanza tuna misitu mingi mfano msitu wa Buhindi uliopo Halmashauri ya Buchosa ambao kwa sasa tunataka maeneo ya aina hii yatumike vyema kuwanufaisha vijana, kwani ni fursa inayoweza kutengeneza ajira,” alisema Elikana.
Aidha, alibainisha hivi karibuni mkoa huo ulikuwa mwenyeji wa Maadhimisho ya Siku ya Ziwa Victoria yaliyolenga kuhimiza jamii umuhimu wa utunzaji na uhifadhi wa mazingira katika ziwa hilo ambalo lina mchango mkuwa katika shughuli za kijamii na kiuchumi.
“Maadhimisho haya ni sehemu ya utekelezaji wa azimio la Jumuiya ya Afrika Mashariki kupitia kamisheni ya bonde la ziwa Victoria…..tulikuwa na matukio mbalimbali ikiwemo zoezi la upandaji miti takribani 2,500 katika eneo la mradi wa maji Butimba” alieleza.
Kwa upande wake, kiongozi wa timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Afisa Misitu Mwandamizi, Lucas Sabida, aliupongeza mkoa wa Mwanza kwa juhudi za kuhamasisha jamii kuhifadhi na kutunza mazingira.
Aidha, alieleza Ofisi ya Makamu wa Rais imeendelea kupata ushirikiano wa kutosha kutoka kwa wataalamu wa mazingira ya mkoa huo na kuufanya kuwa ni miongoni mwa mikoa ya mfano katika uhamasishaji wa jamii juu ya uhifadhi wa mazingira.
Timu ya Wataalamu ya Ofisi ya Makamu wa Rais ipo Mwanza kuratibu maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani Mkoani humo yatakayofanyika Mei 30, 2026.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo anatarajia kuwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda. Maadhimisho hayo yamebeba kaulimbiu isemayo, “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania”.



