NASRA KITANA,Dar Na FRED ALFRED, Dodoma
SERENGETI Boys imekuwa gumzo kila kona huku Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ametoa shilingi milioni 500 kwa timu hiyo ya vijana chini ya umri wa miaka 17, baada ya kutinga fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON U17) na kufuzu Kombe la Dunia, michuano itakayofanyika mwaka huu nchini Qatar.
Pia, ametoa ndege kwa ajili ya kuwafuata wachezaji hao baada ya kumalizika kwa mchezo wa fainali ya kusaka Ubingwa wa kwanza wa Afrika dhidi ya Senegal utakaochezwa Jumanne ijayo.
Akizungumza Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba alisema Rais Dk. Samia amewapongeza wachezaji hao kwa hatua kubwa waliofikia na kuweka historia katika nchini.
“Kutokana na juhudi za vijana hao katika mashindano hayo makubwa, Rais Samia ametoa kiasi cha Milioni 500 baada ya kutinga fainali na endapo watachukua ubingwa wa mashindano hayo, basi kila mmoja atapewa kiwanja mkoani Morogoro ili iwe kumbukumbu kwao.
“Pia, Rais Samia ametoa ndege ambayo itasafiri na baadhi ya watu kwa ajili ya kwenda kuwapa sapoti wachezaji hao na kurejea nao nchini,” alisema Nchemba.
WaziriMkuu alitoa wito kwa Watanzania kuhakikisha wanaendelea kuongeza motisha kwa wachezaji ili waweze kwenda kupigania taifa na kuipeperusha vyema bendera ya nchi.
Timu hiyo inayonolewa na kocha Elieneza Nsanganzelu, imetinga hatua hiyo baada ya kuwaondoa Misri kwa mikwaju ya penalti 4-3, baada ya sare ya kutofungana katika dakika 90 za mchezo wa nusu fainali uliochezwa Uwanja wa Moulay El Hassan Jijini Rabat nchini Morocco.
“Ninaipongeza timu ya Taifa ya Vijana ya Mpira wa Miguu chini ya miaka 17 (Serengeti Boys), kwa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia Mwaka huu.
Mafanikio haya ni fahari kubwa kwa taifa letu ni ushahidi wa vipaji, juhudi na nidhamu ya vijana wetu kuipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa,” alisema.
Aliongeza “Ninawatakia kila la kheri katika mashindano ya Mataifa ya Afrika yanayoendelea. Nimeielekeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na mamlaka zote zinazohusika kuhakikisha maandalizi bora yanafanyika muiwakilishe vyema nchi yetu,” aliandika Rais Dk. Samia.
WENGER
Aliyewahi kuwa kocha wa Arsenal ya England, Arsene Wenger, ameipongeza Serengeti Boys kwa hatua kubwa waliyofikia na kiwango cha kuvutia kilichoipa ushindi katika mchezo huo.
Kocha huyo ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Soka katika Shirikisho la Mpira wa Miguu la Kimataifa (FIFA), pia ameipongeza timu ya Misri na kueleza kwamba anazisubiri timu zote mbili katika michuano ya Kombe la Dunia kwa vijana wa umri huo itakayofanyika nchini Qatar, kuanzia Novemba 19 hadi Desemba 13, mwaka huu.
Huu unakuwa mwaka mzuri kwa Serengeti Boys, ikiweka rekodi nyingine ya kwenda fainali baada ya kuvuka hatua ya makundi kwa mara ya kwanza sambamba na kufuzu Kombe la Dunia.
WABUNGE WATOA AZIMIO
WABUNGE wamepitisha azimio maalumu la kuipongeza Timu ya Taifa ya Vijana chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’ kwa kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika kwa vijana (AFCON 2026) na kukata tiketi ya kushiriki Kombe la Dunia la Vijana mwaka 2026.
Akisoma azimio hilo bungeni jijini Dodoma, jana, Mbunge wa Bunda Mjini (CCM), Ester Bulaya, alisema Bunge linaipongeza timu hiyo kwa kufanya vizuri michuano ya AFCON inayoendelea nchini Morocco.
Alisema Serengeti Boys wameonyesha kiwango kikubwa cha ushindani, uzalendo na nidhamu, jambo lililowapa matumaini Watanzania wengi kuhusu mustakabali wa soka la vijana nchini.
Mbunge wa Makete (CCM), Festo Sanga, alisema mafanikio ya Serengeti Boys ni ushahidi kuwa Tanzania ina hazina kubwa ya vipaji vya michezo vinavyohitaji kuendelezwa na kulindwa.
Alimuomba Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, kuendelea kuchapa kazi huku akisisitiza umuhimu wa kuwaandaa vijana hao kisaikolojia na kuwalinda dhidi ya mameneja na mawakala uchwara.
Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Husna Saiboko, alisema mafanikio ya Serengeti Boys yametokana na uwekezaji mkubwa wa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, katika sekta ya michezo kupitia ujenzi wa viwanja na kuanzisha akademi za michezo Kigamboni na Tanga.
Naye Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Silvia Kigua, alisema ushindi wa Serengeti Boys umefungua matumaini mapya kwa vijana wengi nchini kwa kuonesha kuwa michezo inaweza kuwa chanzo kikubwa cha ajira.
“Ushindi huu haujaja kwa bahati mbaya. Ni matokeo ya maono ya Rais Dk. Samia ambaye ameendelea kuwekeza katika michezo na maendeleo ya vijana,” alisema Kigua.
Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Khadija Hassan Aboud, alisema mafanikio hayo yanaonesha Serikali ilivyojikita kuimarisha sekta ya michezo, huku Mbunge Ester Matiko akisema kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita, michezo imekua kwa kasi kubwa na kuanza kuchochea mafanikio ya kimataifa.
MAKONDA AAHIDI MAKUBWA
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, alimpongeza Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa upendo wake kwa watoto wa Kitanzania kupitia uwekezaji mkubwa alioufanya katika sekta ya michezo.
Makonda alisema Serengeti Boys ni matokeo ya mashindano ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) na vituo vya kukuza vipaji vya michezo vilivyopo Kigamboni na Tanga.
Alisema Serikali imejipanga kuhakikisha Serengeti Boys wanaendelea kupata maandalizi bora na mara baada ya AFCON, watawekwa kambini mapema kwa maandalizi ya Kombe la Dunia.
Aidha, aliwahakikishia wabunge kuwa Serikali haitaruhusu vijana hao kuingia mikononi mwa mameneja na mawakala uchwara; badala yake wataendelea kulelewa kupitia mifumo rasmi ya maendeleo ya michezo.
RUNINGA KUBWA
Pia, Makonda amewaomba wakuu wa mikoa kufunga runinga kubwa siku ya Jumanne kwa ajili ya wananchi kushuhudia mchezo wa fainali kati ya Serengeti Boy na Senegal.
MAFANIKIO SERENGETI BOYS
Mafanikio hayo yanakuja Tanzania ikishiriki kwa mara ya tatu AFCON U17, baada ya mwaka 2017 nchini Gabon na 2019 nyumbani, ambako mara zote walitolewa katika hatua ya makundi.
Katika safari yao ya kuelekea nusu fainali, timu hiyo ilishinda mechi zake katika hatua ya makundi ambapo ilizichapa Msumbiji na Angola kwa mabao 3-0 kila mmoja, kabla ya kuteleza kwa kufungwa mabao 2-1 na Mali.
Ilitinga hatua ya robo fainali kwa mikwaju ya penalti dhidi ya Algeria baada ya kutoka sare ya mabao 3-3.
Serengeti Boys sasa itashuka dimbani Jumanne ijayo kucheza na Senegal katika mchezo wa fainali wa michuano hiyo.
KAMBI
Waziri Makonda alisema jana kuwa Rais Samia ameelekezo vijana wa Serengeti Boys baada ya mashindano ya AFCON 2027 watapelekwa katika Akademi za kimataifa kwa ajili ya maandalizi ya Kombe la Dunia 2030.



