Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema serikali itaendelea kulinda uhuru wa kuabudu na kuimarisha ushirikiano na taasisi za dini kwa kutambua mchango mkubwa unaotolewa na taasisi hizo katika kujenga maadili, amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.
Dk. Mwigulu alisema hayo Mjini Kiomboi, wilayani Iramba, mkoani Singida, aliposhiriki ibada katika Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Kiomboi Christian Centre.
Ibada hiyo iliongozwa na Askofu wa Jimbo la Singida Kaskazini, Dk. Danford Obadia na Mchungaji Kiongozi wa kanisa hilo, Yona Essya.
Akizungumza na waumini hao, Waziri Mkuu, alisema serikali inatambua nafasi muhimu ya taasisi za dini katika malezi ya jamii na itaendelea kuweka mazingira rafiki yatakayowezesha taasisi hizo kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na ufanisi.
“Sisi wote tutaendelea kulinda mazingira bora ya kuendesha ibada. Serikali itaendelea kutambua na kuamini kazi inayofanywa na taasisi za dini katika kujenga taifa letu,” alisema.
Alisema taasisi za dini zimekuwa mshirika muhimu wa serikali katika kujenga maadili mema, kuhimiza uwajibikaji, kuimarisha mshikamano wa kijamii na kupambana na vitendo vinavyokinzana na utu na maendeleo ya wananchi.
Waziri Mkuu alisema Kanisa la TAG, limekuwa na mchango mkubwa katika kuelimisha jamii, kuondoa imani potofu na kuhamasisha wananchi kuzingatia maadili na misingi sahihi ya maisha.
“TAG haikusimama katika ibada pekee, bali imebadilisha hata maisha ya kila siku ya wananchi. Imechangia kuondoa baadhi ya mila na imani zilizokuwa zinarudisha nyuma maendeleo ya watu wetu,” alisema.
Wakati huohuo, Dk. Mwigulu alitoa rai kwa wananchi kuendelea kuheshimu nyumba za ibada na kuepuka kuziingiza katika shughuli
zinazoweza kuvuruga dhamira na malengo yake ya msingi.
“Ukitaka siasa anzisha chama cha siasa. Usipeleke fujo katika nyumba ya ibada. Lazima tuendelee kuheshimu utakatifu wa nyumba zetu za ibada,”alisema.




