Na ATHNATH MKIRAMWENI
SERIKALI imesema haitovumilia vitendo vyovyote vitakavyohujumu utekelezaji wa miradi ya umma ikiwemo rushwa, ukiukwaji wa utaratibu na matumizi mabaya ya rasilimali.
Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, alipozungumza katika mkutano kati ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), wakandarasi na wadau wa miradi ya nishati vijijini.
Alisema kila mdau anapaswa kuhakikisha miradi ya umeme inatekelezwa kwa uwazi, ufanisi, kuzingatia thamani ya fedha ili wananchi wanufaike na uwekezaji mkubwa unaofanywa na serikali katika sekta ya nishati.
Alisema Tanzania imepiga hatua kubwa katika upatikanaji umeme ambapo huduma hiyo, imefikia asilimia 85 kitaifa na asilimia 78 maeneo ya vijijini, hivyo mafanikio hayo, yanatokana na uwekezaji uliofanywa na serikali chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
“Umeme siyo anasa, ni hitaji muhimu na kichocheo kikubwa cha maendeleo ya taifa katika karne hii.
“Hatuwezi kufikia malengo yetu ya maendeleo bila kuwa na umeme wa uhakika unaowafikia wananchi na maeneo ya uzalishaji,” alisema.
Alisema mafanikio ya sekta ya nishati, yanaendana moja kwa moja na maono ya taifa ya kujenga uchumi wa kisasa, shindani na jumuishi kama yalivyoainishwa katika Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.
Alisema lengo la serikali siyo kusambaza umeme pekee, bali kuhakikisha unatumika kuchochea viwanda, kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, kuibua ajira kwa vijana na kuvutia uwekezaji wenye tija.
Waziri huyo, alisema bado kuna changamoto ya kiwango cha matumizi ya umeme kiko chini ya matarajio, licha ya wananchi wengi kufikiwa na huduma hiyo.
Alieleza kuwa, kiwango cha matumizi ya umeme kitaifa ni asilimia 52.1 huku vijijini kikiwa asilimia 37.1, jambo linalohitaji jitihada za kuhamasisha matumizi yenye tija katika sekta za kilimo, uvuvi, biashara na viwanda vidogo.
Ndejembi aliwataka REA, wakandarasi na wasimamizi wa miradi, kushirikiana kwa karibu na vyombo vya ulinzi na usalama kulinda vifaa vya umeme vinavyosafirishwa na kufungwa katika maeneo mbalimbali, kuzuia wizi unaosababisha hasara kwa serikali na kuchelewesha huduma kwa wananchi.
“Umeme siyo anasa, unapochelewesha kufika kwa wananchi, unachelewesha maendeleo yao. Hatuwezi kuruhusu vifaa vya miradi kuibiwa na kazi kuchelewa kukamilika bila hatua kuchukuliwa,” alisema.
Ndejembi aliwapongeza wakandarasi waliotunukiwa tuzo kwa kukamilisha miradi kwa wakati na viwango vinavyotakiwa.
MKURUGENZI MKUU REA
Mkurugenzi Mkuu wa REA, Hassan Saidy, alisema utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, umeendelea kuimarika nchini.
Alisema kandarasi 32 kati ya zaidi ya 150 zinazotekelezwa chini ya miradi mikubwa 13, tayari zimekamilika.
Hatua hiyo, imewezesha vitongoji 6,954 kati ya 7,431 vilivyokuwa katika hatua za utekelezaji, kuunganishwa na huduma ya umeme, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kufikisha umeme katika vitongoji zaidi ya 17,000 nchini.
Alisema mafanikio hayo, yametokana na usimamizi madhubuti, uwajibikaji wa wakandarasi na ushirikiano wa karibu kati ya REA, Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na wadau wa sekta ya nishati.




