NA MUSSA YUSUPH,
Bahi
MGOMBEA Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema serikali inafanya uhakiki wa madai ya fidia kwa wananchi waliopisha mradi wa reli ya mwendokasi (SGR) na miradi mingine ya maendeleo wilayani Bahi, mkoani Dodoma.
Dk. Samia aliyasema hayo katika mkutano wa kampeni uliofanyika wilayani hapo, alipokuwa njiani kwenda mkoani Singida.
“Ninatambua kuna madai ya fidia kwa waliopisha mradi wa SGR, lakini na miradi mingine. Madai yenu tunayafanyia uhakiki na tutakapomaliza, fidia zinakwenda kulipwa,” alisema Dk. Samia.
Kuhusu ujenzi wa reli hiyo, alieleza katika awamu ya pili kutajengwa kituo cha abiria na bandari kavu.
Alisema ujenzi wa kituo na bandari kavu utaongeza kasi ya maendeleo katika wilaya hiyo.
“Ujenzi wa kituo na bandari kavu unakwenda kuibadilisha Bahi kwa sababu vitavutia uwekezaji, biashara na kuchochea ongezeko la ajira.
“Miaka mitano mbele tunakokwenda yanakuja makubwa zaidi na wanasema yajayo yanafurahisha. Hiyo ndiyo dhamira yangu ya kusimama kuwaomba ikifika Oktoba 29, mwaka huu, wote tukapige kura,” alieleza.
Akizungumzia huduma za afya, Dk. Samia alisema serikali imejenga hospitali ya wilaya, vituo vya afya na zahanati.
Kwa upande wa elimu, alisema katika kipindi cha miaka mitano, serikali imejenga shule mpya za msingi 14, hivyo jumla kufikia 86.
Alieleza kwa shule za sekondari, serikali imejenga shule tatu mpya hivyo kufikisha 25 katika wilaya hiyo huku akisisitiza mpango uliopo kujenga mabweni ya wanafunzi wa kike.
“Pamoja na hayo, tumejenga vyuo viwili vya VETA vyenye wanafunzi 156 ambao wanakwenda kujifunza fani za ujenzi, ushonaji, kompyuta, ufundi umeme wa majumbani na magari.
“Na hizi ndizo kazi zitakazowatoa vijana wetu kwa sababu wapo mijini na katika njia kubwa. Tutafikiria baadaye kuanzisha fani ya kilimo na ufugaji,”aliongeza Dk. Samia.




