Na NJUMAI NGOTA,
Rukwa
BAADHI ya wakazi wa Mkoa wa Rukwa, wameahidi kumpatia kura za kishindo Mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, kutokana na kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025, hasa katika sekta za afya, elimu, miundombinu na maji safi na salama.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mikutano ya kampeni za CCM iliyofanyika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Vijijini na Kalambo, wananchi hao, walionesha kuridhishwa na kasi ya maendeleo yanayotekelezwa chini ya uongozi wa Dk. Samia.
Mkazi wa Kalambo, Khadija Selemani, alisema miaka mitano iliyopita, kulikuwa na changamoto kubwa katika upatikanaji huduma za kijamii, hivi sasa, hali imebadilika kwa kiasi kikubwa, kutokana na msukumo wa Serikali ya Awamu ya Sita.
“Hivi sasa huduma ya maji safi na salama inapatikana. Dawa zinapatikana hospitalini na watumishi wa afya, wanawahudumia wagonjwa kwa upendo. “Hatuna cha kumlipa Mama Samia zaidi ya kumpigia kura nyingi za kishindo Oktoba 29,” alisema.
Alieleza kuwa, barabara nyingi zimeboreshwa kwa kiwango cha changarawe na nyingine kuwekwa lami, hivyo wanaamini wagombea wa CCM wataendelea kukamilisha maeneo machache yaliyosalia.
“Dk. Samia anatatua matatizo ya wananchi kwa vitendo, tunamwomba aendelee na kazi hii nzuri ya kulijenga taifa na kukuza uchumi wetu,” alisema.
Naye, mkazi wa Laela, John Sangu, aliwaomba Watanzania kujitokeza kwa wingi Oktoba 29 na kumpigia kura Dk. Samia pamoja na wabunge na madiwani wa CCM, huku akisema maendeleo yaliyopatikana Rukwa ni dhahiri na hayahitaji maelezo marefu.
“Barabara hivi sasa zinapitika muda wote, huduma za afya, zimeboreshwa na shule nyingi zimejengwa. Watoto wetu wanakaa katika madawati na ufaulu umeongezeka, hiyo inatokana na dhamira ya dhati ya Dk.Samia, kutoa elimu bure,” alisema Sangu.
Kabula Mashimo, alisema amejiandaa kushiriki uchaguzi huo kwa kuwapigia kura wagombea wanaotokana na Chama Cha Mapinduzi.
“Tunahitaji kila Mtanzania atoke Oktoba 29 akakipigie kura Chama chetu ambacho kimeendelea kutupatia maendeleo kupitia utekelezaji wa Ilani ya CCM,” alisema.
Alisema wanawake nchini, wana kila sababu ya kumuunga mkono Dk. Samia kutokana na jitihada zake katika kuwaondolea adha ya kubeba ndoo za maji kichwani kwa kuwasogezea huduma karibu na makazi yao na kuwawezesha kupata nishati safi ya kupikia.




