Na LILIAN JOEL,
Arusha
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba amesema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ameliagiza Jeshi la Polisi nchini, kuacha kumtafuta Askofu Dk. Josephat Gwajima kama walivyokuwa wametangaza awali, aendelee na shughuli zake.
Amesema baada ya kutoa msamaha kwa Kanisa la Ufufuo na Uzima, waumini wanahitaji wamuone kiongozi wao, hivyo anatakiwa ajitokeze hadharani aendelee na kazi yake.
“Mwacheni ajitokeze tujenge umoja wa kitaifa, tushikamane kurudisha umoja wa kitaifa. Tumekutana na TEC, viongozi wa dini, wa mila na viongozi mbalimbali; twendeni sote katika jambo hili, tujitokeze tuhamasishe Tanzania yenye amani, huu ndiyo wito wa kiongozi wetu wa nchi,” alisema Waziri Mkuu, Dk. Nchemba, jana.
Waziri Mkuu Dk. Nchemba alisema hayo, alipozungumza na mamia ya wakazi wa Arumeru katika mkutano wa hadhara uliofanyika Uwanja wa Magufuli Leganga, Kata ya Usa River, wilayani Arumeru, mkoani Arusha.
Aliwataka Watanzania wakatae kushawishiwa na wanaharakati wanaochochea vurugu kwa kuwa zinarudisha nyuma maendeleo ya nchi.
“Nimekuja kuwapa pole wananchi wenzangu kwa niaba ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan. Anatambua mambo yanayoendelea. Anatambua kazi kubwa ya kujenga Taifa mnayoifanya,” alisema.
Kabla ya mkutano huo, Waziri Mkuu alikagua uharibifu uliofanywa katika vurugu za Oktoba 29, mwaka huu katika Kituo cha Polisi cha Kikatiti (mita 500 kutoka Barabara Kuu ya Arusha – Moshi); Mahakama ya Mwanzo ya Maji ya Chai (kilometa tatu kutoka barabara hiyo kuu); kituo cha mafuta Total Energies kilichopo Maji ya Chai (kipo barabarani), ambapo vilichomwa moto, ikiwemo kuiba mali katika ‘supermarket’ na kubomoa sefu ya kutunzia fedha.
Waziri Mkuu alisema masuala ya maendeleo ya wilaya hiyo, yakiwemo maji na barabara yamo katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ahadi za Rais, lakini yatafanyika endapo nchi itakuwa na amani.
“Tukichagua vurugu tutakuwa tumechagua kufukuza maendeleo, tukichagua vurugu tutakuwa tumechagua kuongeza umaskini kwa mtu mmoja mmoja,” alionya.
Aliongeza kuwa: “Kila Mtanzania akatae haya yaliyotokea juzi juzi. Tumechochewa, tumechonganishwa, lakini wao wako nje, wanalipwa kutuvuruga tu. Wengi wanaochochea vurugu ni wanaharakati, wako nje ya nchi. Hakuna kiongozi wa chama cha siasa anasema wananchi wafanye vurugu. Au mmemuona?,” alihoji.
Alisema baadhi ya vijana walioko nje ya nchi wamebainika kupokea dola za Marekani milioni mbili (sawa na sh. bilioni 4.5) wachochee vurugu.
“Hawa wanaowalipa wana maslahi gani na nchi yetu? Wana ajenda gani na nchi yetu? Tunajua watazirudishaje hizo fedha?.”
“Hawa watu wanalenga tugombane wachukue madini adimu (rare earth minerals). Hivi sasa Tanzania imegundua uranium ambapo inakuwa nchi ya tisa duniani na ya kwanza barani Afrika. Ina tani za ujazo 890,000. Hii ni karibu na tani milioni moja,” alisema.
Waziri Mkuu alionya dhidi ya mchezo unaotumika kuanzisha chokochoko kusambaratisha nchi pindi inapobainika kuwa na rasilimali.
Alisema ziko baadhi ya nchi barani Afrika ziliathirika kutokana na chokochoko hizo.
“Wanaanzisha chokochoko, wanaacha mnavurugana, rasilimali zikiisha, wao wanaondoka. Watanzania tuamkeni, tuchukue tahadhari. Kuna kamchezo kanachezwa. Wanajua Tanzania ina gesi asilia nyingi na inakaribia kuanza. Wanajua ikianza miradi hii, Tanzania itakuwa ya kwanza katika Afrika Mashariki na wala hatutahitaji kutoa mikopo ya wanafunzi,” alisema.
Aliwataka Watanzania waamke na kukataa kurudishwa tena katika hali ya vurugu.
“Watanzania tuamke, tukatae kurejeshwa kule nyuma. Umaskini utaondolewa nchi ikiwa katika amani. Ajira za vijana zitapatikana nchi ikiwa katika amani,” alisema.
Alisisitiza vurugu zikiwepo, hata wakulima wa karoti na nyanya wa Ngarenanyuki hawatauza, hivyo kuathiri uchumi wa mtu binafsi.




