AMINA KASHEBA
KOCHA wa ngumi za kulipwa, Kanda Kabongo amewataka mashabiki wa bondia, Hassan Mwakinyo kuwa na imani naye kuelekea katika pambano la ‘Boxing On Boxing Day’.
Mwakinyo atapanda ulingoni Desemba 26, mwaka huu, ukumbi wa Superdome, Dar es Salaam katika pambano hilo ambalo mpinzani wake bado hajawekwa hadharani.
Akizungumza Dar es Salaam, Kabongo alisema asilimia kubwa ya mazoezi ya Mwakinyo yamekamilika, hivyo aliwaomba Watanzania wategemee mambo mazuri kutoka kwake.
“Mwakinyo kila siku anafanya mazoezi ndiyo maana sina wasiwasi na yeye kwa sababu mimi ndiye napanga programu nzima ya mazoezi yake.
“Pia, tumekuwa tukifanya mazoezi kabla ya kutangazwa pambano hilo kwa sababu ngumi ndiyo mchezo wake, hivyo Watanzania wategemee mambo mazuri kutoka kwa Mwakinyo,” alisema.
Kocha huyo alisema mbali ya mpinzani wake kutofahamika hadi leo, bado ana imani atapambana na b ondia mwenye uwezo mkubwa.
Mkurugenzi wa Peak time Media, Meja Selemani Semunyu ambao ni waandaji wa pambano hilo, alisema mpinzani wa Mwakinyo atafahamika muda wowote ndani ya wiki hii.
“Tupo katika upangaji wa orodha ya mabondia ambao watapanda ulingoni katika pambano la ‘Boxing On Boxing Day’, pia wiki ijayo Watanzania watafahamu mpinzani wa Mwakinyo, ambaye atakuwa (main card),”alisema.
Meja huyo aliongeza kuwa milango ya kudhamini pambano hilo, ipo wazi kwa kampuni, taasisi za umma na binafsi.




