Na AMINA KASHEBA
PAMOJA na kushinda kwa TKO bondia wa ngumi za kulipwa, Mtanzania Emmanuel Mwakyembe, amempongeza mpinzani wake Tionge Chingeni kutoka Malawi kwa kuonyesha ushindani mkubwa katika pambano hilo.
Mwakyembe alimchapa Chingeni kwa TKO raundi ya tano, mwishoni mwa wiki katika pambano la ‘Punch to Punch’, lisilo la ubingwa uzito wa kati lililofanyika Ukumbi wa The Sea View Dome Banguel uliopo Kawe, Dar es Salaam.
Akizungumza Dar es Salaam, bondia huyo alisema mpinzani wake alionyesha ushindani mkubwa hatua ambayo ilifanya pambano hilo kuwa zuri.
Mwakyembe alisema ubora wa mpinzani wake ulimfanya kutumia muda mwingi kufikiria mbinu za kumchapa hadi alipofanikiwa katika raundi ya tano.
Pia, bondia huyo aliwashukuru Watanzania kwa kumuunga mkono katika pambano hilo.
“Haikuwa rahisi lakini nguvu ya Watanzania imeonekana maana wao wamenipa hamasa ya kupambana hadi nikapata ushindi kwa sababu mpinzani wangu alikuwa na nguvu na mgumu kupigika kwa urahisi.
“Ninashukuru Mungu nimetimiza ahadi ya kuwapa zawadi ya furaha Watanzania kwa kupata ushindi wa kishindo, hii inaniongezea kuaminika kwa kwa mashabiki zangu,” alisema.
Promota wa pambano hilo, Latifa Jabiri alisema mwisho wa mtanange huo ndiyo mwanzo wa pambano lingine, hivyo wadau wa masumbwi wategemee mambo mazuri kutoka kwa kampuni yake ya Three Sports Promotion.




