Na AMINA KASHEBA
SERIKALI imepanga kukutana na wadau wa mchezo wa pooltable kujadili namna ya kunyanyua timu za taifa za mchezo huo kufanya vyema kimataifa.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma, alisema serikali itakaa na wadau mbalimbali ikiwemo Chama cha Pooltable Tanzania (TAPA) kuhakikisha mchezo huo unafanya vyema zaidi.
Mwinjuma alisema timu ya taifa ya mchezo huo imekuwa ikifanya vyema ikiwemo hivi karibuni kushika nafasi ya pili katika Kombe la Afrika hivyo serikali itaongeza nguvu kuhakikisha inafanya vizuri zaidi.
“Moja kitu kilichonifurahisha ni namna ya viwango vya wachezaji vimekuwa vikubwa, nimesikia timu ya taifa ilishika nafasi ya pili mara mbili mashindano ya Afrika ni muda wa serikali kuangalia kwa macho mawili kwa sababu kuna vijana wana uwezo wa kuwa mabingwa,” alisema.
Mwinjuma alisema serikali itaongeza nguvu kuhakikisha hakuna ukata wa mara kwa mara kwa timu zinapokwenda kushiriki michuano mbalimbali.
Pia, alisema serikali ina mpango wa kuweka maeneo maalumu kwa ajili ya kuchezwa mchezo huo.
“Mchezo wa Pooltable mara nyingi unachezwa mtaani, hivi sasa umekuwa ukifanya vizuri kwa timu ya taifa, sasa ni muda wa ushirikiano kati ya serikali na viongozi wa mchezo kuona namna ya kusaidia kufika mbali zaidi kwani uwezo wa kuchukua ubingwa upo,” alisema.




