ABDUL DUNIA Na AMINA KASHEBA
WAKATI Kocha Miguel Gamondi akisisitiza timu ya taifa ‘Taifa Stars’ ipo tayari kushindana katika Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, ubora wa wapinzani wake unamweka mtegoni kukiongoza kikosi chake kuvunja mwiko wa kutovuka makundi.
Katika michuano hiyo iliyoanza jana nchini Morocco, Taifa Stars imepangwa kundi C na Nigeria, Tunisia na Uganda.
Hiyo ni mara ya nne kwa Tanzania kushiriki katika fainali za AFCON, ikianza mwaka 1980, 2019 na 2023.
Hata hivyo, Stars ndiyo timu pekee katika kundi hilo ambayo haijawahi kuvuna pointi tatu wala kutinga hatua ya mtoano, ambapo mara zote tatu zilizopita iliishia makundi huku wapinzani wake wakipata mafanikio mbalimbali.
Nigeria iliyokata tiketi ya kushiriki mara 21 imetwaa ubingwa mara tatu (1980, 1994 na 2013), Tunisia iliyoshiriki mara 22 imebeba ‘ndoo’ hiyo ya Afrika mwaka 2004 na Uganda iliyoshiriki mara nane ikimaliza nafasi ya pili mwaka 1978.
Katika michuano ya mwaka huu, Gamondi raia wa Argentina, atakuwa na kibarua kizito kuhakikisha timu hiyo kwanza inavunja rekodi kwa kupata ushindi wake wa kwanza na pia kutinga mtoano kwa mara ya kwanza katika historia.
Akizungumzia ubora wa kikosi chake na wapinzani wake wiki iliyopita, Gamondi alikiri michuano hiyo ni mikubwa Afrika lakini anaamini timu yake ipo tayari kwa kushindana na kufanya vyema.
“Tunajaribu kuboresha uwezo wa wachezaji mmoja mmoja na kimbinu, ninafikiri wachezaji wanaelewa na ninafurahia kuona wachezaji wakijitoa sana mazoezini.
Tunakwenda kucheza na timu bora Afrika, itakuwa (michuano) migumu sana lakini tupo tayari kwa ushindani,” alisema.
Hoja hiyo iliungwa mkono na beki wa timu hiyo, Dickson Job, ambaye alidai kuwa, hiyo ni fursa kwa kila mchezaji kuonyesha kiwango kikubwa kujitangaza.
“Haya ni mashindano makubwa sana Afrika na sisi kama wachezaji hii ni nafasi yetu kuonyesha kiwango kikubwa, tunakwenda kupambana kuhakikisha tunapata matokeo mazuri,” alisema.
NINI CHA KUFANYA?
Wakati rekodi ya Tanzania kutofanya makubwa AFCON ikimweka mtegoni Muargentina Gamondi, makocha wa soka nchini wanaamini kama Taifa Stars itafanya mambo sahihi kwa wakati sahihi basi hakuna kitakachoshindikana.
Kocha wa Mbeya City ya Ligi Kuu Tanzania Bara, Mecky Mexime alisema kitu kikubwa ambacho Stars inapaswa inapaswa kujiandaa vyema kimbinu kuhakikisha inashinda katika mechi zake.
“Katika mpira lolote linatokea hata kama timu hapo zamani ilikuwa na historia nzuri inaweza kufungwa muhimu ni namna ya kujipanga kuhakikisha unapata ushindi katika kila mchezo,” alisema.
Kocha huyo wa zamani wa Kagera Sugar, alisema ushirikiano baina ya wachezaji na benchi la ufundi ni miongoni mwa sababu muhimu ambayo inaweza kuongeza makali katika kikosi dhidi ya miamba kama Nigeria na Tunisia.
Aliyekuwa kocha wa Yanga na Ruvu Shooting, Charles Mkwasa, alisema usikivu wa wachezaji juu ya mbinu za benchi la ufundi ni miongoni mwa sababu ya msingi inayoweza kuibeba Stars katika fainali za AFCON mwaka huu.
“Wachezaji wa Stars wafuate yale wanayoambiwa na benchi la ufundi, ninaamini wakishirikiana vyema watafanikiwa,” alisema.
Salvatory Edward ambaye aliwahi kuwa kocha msaidizi wa Pamba Jiji, alisema umakini, kujitoa na usikivu mzuri wa mbinu za benchi la ufundi itakuwa silaha bora kwa Taifa Stars katika fainali hizo.
“Stars inapaswa kuzingatia umakini, kujitoa na kusikiliza maelekezo ya walimu, wakifuata hayo na wakishirikiana vyema basi watapata mafanikio makubwa na kufika mbali katika mashindano ya AFCON,” alisema Edward.
Kocha na mchambuzi wa soka, Kennedy Mwaisabula maarufu Mzazi, alikiri Stars kuwa katika kundi gumu, lakini anaamini kama wachezaji watasikiliza vyema mipango ya makocha basi hakuna kitakachowazuia kufanya vyema.
“Stars ipo katika kundi gumu kwa sababu timu inazocheza nazo zina viwango vya juu, hivyo umakini unahitajika mfano timu kama Uganda ina wachezaji wengi ambao wanacheza soka la kulipwa Ulaya bado Nigeria na Tunisia,” alisema.




