Na AMINA KASHEBA
KOCHA wa Yanga Princess, Edna Lema maarufu Mourinho, amesema anafurahishwa na ubora wa kikosi chake unaoonyeshwa sasa katika mechi za Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania Bara.
Edna ametoa kauli hiyo baada ya Yanga Princess kupata ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Geita Queens katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam.
Kutokana na ushindi huo, Yanga Princess ipo kileleni mwa msimamo ikiwa na pointi 12 wakati nafasi ya pili ikishikwa na Simba Queens yenye pointi 12 wakitofautiana mabao wakati JKT Queens ikiwa nafasi ya tatu kwa pointi 10, zote zikishuka dimbani mara nne.
Kocha huyo amesema wachezaji wake wamekuwa na kiwango kizuri hivi sasa kutokana na kufuata vizuri maelekezo anayowapatia.
“Timu imebadilika kwa kiwango kikubwa, ninaona mabadiliko kwa mtu moja moja, kitu ambacho nimefarijika kuona wachezaji chipukizi kufanya vizuri baada ya kuwapa nafasi ya kucheza,” amesema.
Kocha huyo ameongeza kuwa, kikosi chake kimekuwa na wakati nzuri msimu huu kutokana na kuwa na umakini mzuri katika kutumia nafasi.
Mchezaji wa Yanga Princess, Jeaninne Mukandayisenga, alisema malengo yao ni kuchukua ubingwa wa ligi hivyo na anaamini inawezekana kwani watapambana kuhakikisha wanapata ushindi katika mechi zao.
“Tutahakikisha tunapambana kupata ushindi katika kila mechi, malengo yetu ni kuchukua ubingwa wa ligi tunatambua kuna ushindani kubwa, tumejipanga,” amesema.




