Na MWANDISHI MAALUMU
SERIKALI ya Saudi Arabia imesema itaendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuimarisha uhusiano zaidi katika nyanja mbalimbali.
Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje ya Ufalme wa Saudi Arabia, Waleed bin Abdulkarim El Khereiji, alipopokea ujumbe maalumu kutoka kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, uliowasilishwa kwa Mwanamfalme na Waziri Mkuu wa Saudi Arabia Mtukufu Mohammed bin Salman Al Saud.
Taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya habari na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ilisema ujumbe huo uliwasilishwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo akiambatana na Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Profesa Palamagamba Kabudi.
Akipokea ujumbe huo, Waleed alisema Saudi Arabia inatambua na kuthamini uhusiano wa muda mrefu na imara wa muda mrefu wa kidiplomasia, kibiashara na kiutamaduni uliopo kati ya Ufalme wa Saudi Arabia na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aidha, Waleed aliahidi Ufalme wa Saudi Arabia utaendelea kushirikiana kwa karibu na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Tanzania kwa kuimarisha zaidi maeneo ya vijana, utamaduni, biashaa, uwekezaji, utalii, elimu, ajira na maeneo mengine yaliyoafikiwa na nchi hizo mbili.
Vilevile, alieleza dhamira ya Ufalme wa Saudi Arabia kuunga mkono jitihada uwezeshaji wa vijana zilizowekwa na Serikali ya Tanzania na Waziri Kombo.




