ARUSHA
NA MWANDISHI WETU
MIILI ya watu watano waliofariki dunia baada ya Helkopta ya kampuni ya uokoaji ya Kilimedair kuanguka eneo la Barafu Camp, Mlima Kilimanjaro, imetambuliwa.
Ajali hiyo iliyotokea juzi jioni wakati helkopta hiyo ilipotoka kuchukua wagonjwa katika Mlima Kilimanjaro ikiwa na watu watano.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa, iliwataja watu hao ni Costantine Mazonde raia wa Zimbabwe ambaye alikuwa rubani, Jimy Daniel aliyekuwa daktari na Inocent Mbaga ambaye ni muongoza watalii.
Wengine waliofariki dunia ni Plos David na Plosova Anna ambao ni raia wa Jamhuri ya Czech ambapo walikuwa wamepanda Mlima Kilimanjaro.
“Ndege ya kampuni ya Kilimedair inayofanya kazi za uokoaji Mlima kilimanjaro imepata ajali maeneo ya Bonde la barafu majira ya saa 11:30 jioni, helikopta ilikua na watu watano na wote wamefariki dunia,” alisema Kamanda Maigwa.




