NA MWANDISHI WETU
MAHAKAMA Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi imemuhukumu Iddi Nassoro kifungo cha miaka 25 gerezani baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kukutwa na dawa za kulevya aina ya heroine kilo 1.02.
Nassoro alikamatwa na dawa hizo katika Stendi ya Mabasi Magufuli iliyopo Mbezi akisafirisha kwenda mkoani Tanga ambapo katika kesi hiyo wenzake watatu wameachiwa huru.
Hukumu hiyo ilitolewa mahakamani hapo na Jaji Godfrey Isaya baada ya mahakama kupitia ushahidi wa pande zote mbili.
Baada ya mahakama kupitia ushahidi huo, ilithibitisha shtaka la kusafirisha dawa za kulevya pasipo kuacha shaka dhidi ya mshtakiwa wa pili.
Jaji Isaya alisema mahakama iliona upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mashtaka dhidi ya mshtakiwa wa kwanza Maliki Maliki, Ally Maliki ambaye ni kocha wa mpira wa miguu na Mwingi Mwinyi hivyo iliwaachia huru.
Washtakiwa katika shauri hilo walikuwa wakikabiliwa na mashtaka mawili ambapo katika shtaka la kwanza walidaiwa Machi 24 mwaka 2022 maeneo ya Stendi ya Magufuli Mbezi walikutwa wakisafirisha dawa za kulevya aina ya heroine kilo 1.02 kwenda mkoani Tanga.




