Na ABDUL DUNIA
TIMU ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ leo itashuka dimbani katika dabi ya Afrika Mashariki dhidi ya Uganda maarufu The Cranes.
Mechi hiyo ya aina yake ya kundi C katika Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, itapigwa saa 2:30 usiku katika Uwanja wa Al Medina uliopo Rabat, Morocco.
Mtanange huo ni wa kwanza kwa timu hizo kukutana katika historia ya AFCON, ambapo Tanzania ikifuzu michuano hiyo mara nne na Uganda mara nane.
Tanzania ilianza kampeni yake katika AFCON kwa kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya Nigeria wakati Uganda ikifungwa 3-1 ilipocheza na Tunisia.
Katika michuano mingine na mechi za kuwania kufuzu AFCON, miamba hiyo miwili ya Afrika Mashariki imewahi kukutana mara 61.
Katika mchanganuo huo, Uganda ndiyo kinara wa ubabe ikishinda mechi 33, Tanzania mechi 12 na timu hizo zimetoka sare mara 16.
Hivi karibuni, miamba hiyo ilikutana katika mechi za kuwania kufuzu fainali za AFCON 2023, ambapo Tanzania ilishinda bao 1-0 ugenini na Uganda ilipata ushindi kama huo ugenini.
Katika kundi hilo, Tanzania ilimaliza nafasi ya pili juu ya Algeria na kufuzu fainali hizo zilizopigwa nchini Ivory Coast.
Uhasama wa timu hizo ulianza Septemba 8, 1964 ambapo Tanzania iliifunga Uganda mabao 3-0 katika mchezo wa Kombe la Afrika Mashariki.
Katika vita vya wawili hao, Uganda iliwahi kuweka rekodi ya kuifunga Tanzania kwa mabao 5-0 katika Kombe la CECAFA, Novemba 30, 1991.
Katika AFCON, Uganda imepoteza mechi zote mbili ilizocheza na timu kutoka ukanda wa CECAFA, ambapo ilifungwa mabao 2-1 na 2-0 dhidi ya Ethiopia katika fainali za mwaka 1968 na 1976.
Tanzania nayo ilipoteza 3-2 dhidi ya Kenya katika AFCON mwaka 2019 nchini Misri.
Kiungo wa Uganda, Khalid Aucho (Singida Black Stars) na straika Steven Mukwala (Simba) wanakipiga katika Ligi Kuu Tanzania Bara.
Katika klabu, Aucho ananolewa na Kocha wa Taifa, Miguel Gamondi.
TAKWIMU MUHIMU UGANDA
Kipigo dhidi ya Tunisia wiki iliyopita ni kichapo chao cha 17 katika mechi 24 za AFCON.
Goli la pili ililoruhusu timu hiyo dhidi ya Tunisia lilikuwa goli la 40 kufungwa katika AFCON.
Goli la Denis Omedi dhidi ya Tunisia lilimaliza ukame wa mabao wa zaidi ya dakika 376 katika AFCON kwa miamba hiyo.
Miamba hiyo imeshinda mechi moja kati ya tisa za mwisho katika AFCON.
Tangu ujio wa hatua ya makundi ya AFCON mwaka 1968, Uganda haijawahi kushinda mechi yake ya pili ya kundi, ikipoteza mara nne na kutoka sare mbili.
TAKWIMU TANZANIA
Kichapo cha 2-1 dhidi ya Nigeria ni mechi ya 10 kwa Tanzania kucheza katika AFCON.
Kipigo hicho ni cha saba kwa Tanzania katika fainali hizo, ikitoka sare mara tatu.
Tanzania ni timu ya nne kushinda kushinda katika mechi zake 10 za kwanza za AFCON, ikifuatiwa na Benin (15), Msumbiji (14) na Guinea-Bissau (12).
Charles M’Mombwa ambaye ndiye mfungaji wa bao la Tanzania dhidi ya Nigeria, amefuga mabao matatu katika mechi nne zilizopita za Tanzania katika mashindano yote.
Tanzania imepoteza mechi zote za kwanza ilizocheza katika AFCON.
Katika fainali za mwaka 1980 na 2019, Tanzania ilipoteza mechi zake za pili za kundi.
Katika AFCON 2023, Tanzania ilitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Zambia.
Mechi tisa kati ya 10 ilizocheza Tanzania katika AFCON zimetoa magoli, ni dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) pekee ndiyo iliisha kwa suluhu.
Goli dhidi ya Nigeria limeweka rekodi kwa Tanzania kufunga angalau bao moja katika kila AFCON iliyoshiriki.




