RIYADH, Saudi Arabia
NAHODHA wa timu ya taifa ya Ureno na klabu ya Al Nassr ya Saudi Arabia, Cristiano Ronaldo amesema hatostaafu soka hadi atakapoweka rekodi ya kufunga mabao 1,000.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 40, hivi sasa ana mabao 956 katika maisha yake ya soka baada ya mwishoni mwa wiki iliyopita kufunga mabao mawili katika ushindi wa 3-0 dhidi ya Al Akhdoud katika Ligi Kuu ya Saudi Arabia.
Ronaldo aliyejiunga na Al Nassr mwaka 2022, Julai mwaka huu alisaini mkataba wa miaka miwili kuendelea kukipiga katika timu hiyo hatua ambayo inaweza kumfanya akacheza hadi atakapokuwa na umri wa miaka 42.
Akizungumza baada ya kushinda tuzo ya mchezaji bora wa Mashariki ya Kati katika tuzo za Globe Soccer Awards mwishoni mwa wiki, mkongwe huyo alisema ni ngumu kuendelea kucheza soka lakini bado anaendelea kuhamasika.
“Malengo yangu nataka kushinda mataji na kufikia hiyo idadi (mabao 1,000) ambayo kila mmoja anajua. Nitafikia hiyo idadi kwa hakika, kama sitopata majeraha,” alisema.
Katika mechi 14 alizoitumikia Al Nassr msimu huu, Ronaldo amefunga mabao 13.




