Na IRENE MWASOMOLA
SERIKALI imejipanga kutoa fursa mpya kwa vijana kwa lengo la kuwawezesha kujiajiri na kukuza ujuzi, huku ikitenga jumla ya hekari 170,000 za mashamba na viwanja kuliwezesha kundi hilo kufanya shughuli za uzalishaji.
Pia, imesema imeanzisha vituo maalumu vya ujasiriamali kwa vijana katika mikoa ya Dodoma, Mara, Pwani na Ruvuma, ikiwa ni mwanzo wa utekelezaji wa kuwezesha vijana kujiajiri.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa Jukwaa la Vijana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka alisema serikali imeanza kutekeleza uanzishwaji wa maeneo ya kiuchumi kwa vijana katika meneo mbalimbali nchini ambayo ni maalumu kwa uwekezaji.
Pia Nanauka alisema serikali chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kushirikisha vijana katika zabuni na manunuzi ya serikali ambapo jumla ya zabuni zenye thamani ya sh. bilioni 10.8 zilitolewa kwa vijana katika kipindi cha mwaka jana.
“Serikali imeanza kutekeleza kwa vitendo ajenda ya kuanzisha maeneo maalumu ya kiuchumi kwa vijana, mpango huu ni makakati mahususi wa kuongeza ushiriki wa vijana kuhusika katika uzalishaji,”alisema.
Pia alisema kupitia mpango wa maeneo ya kiuchumi ya uwekezaji kwa vijana, serikali imelenga kuwezesha kuanzisha jumla makampuni 20,000 ambayo yatakuwa katika maeneo ya uwekezaji ambao upo chini ya vijana.
Aidha, akizungumza kuhusu mikopo ya asilimia 10 Nanauka, alisema katika kipindi cha mwaka jana vijana wamenufaika na jumla ya sh. bilioni 36.4 ambazo zilitolewa kama mikopo isiyokuwa na riba.
Aidha Nananuka aliwataka Maofisa Maendeleo ya Vijana wa Mikoa kuhakikisha wanashirikiana na vijana katika maeneo yao katika kutafuta fursa kupitia sekta binafsi.
Pia Nanauka alisema, jukwaa la vijana alilozindua ni la kimkakati ambalo litatoa fursa kwa vijana kusikika, kutoa maoni yao na kupata nafasi ya kujua fursa zilizopo.
Aliongeza kuwa serikali itahakikisha maoni yatakayokuwa yanatolewa kupitia jukwaa hilo yanachakatwa, yana nakiliwa na kufanyiwa kazi kwa wakati.
Nanauka alisema serikali inaendelea kuimarisha ujuzi wa vijana kupitia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), na kukuza ubunifu wa kidijitali.
KATIBU MKUU
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Jenifer Omolo, alisema jukwaa hilo lililozinduliwa linalenga kuhakikisha vijana wanapata nafasi ya kusikilizwa kwa ukaribu.
Pia alisema jukwaa hilo litasaidia vijana kuunganishwa na sekta binafsi, wadau mbalimbali wa maendeleo na kuwasaidia kujua fursa za kiuchumi na kijamii.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo, alisema serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam umeendelea kushirikiana kwa karibu na vijana katika kuzifikia fursa mbalimbali.
Alisema wilaya ya Ilala itaendelea kushirikiana kwa karibu na vijana katika kuhakikisha wanapata maendeleo na kujikwamua kiuchumi, kupitia utoaji wa mikopo ya asilimia 10 na fursa nyinginezo.




