Na FRED ALFRED, Dodoma
MOSHI mweupe wenye ishara ya matumaini, umeanza kufuka Uwanja wa Msalato, baada ya Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, kusema ndege zitaanza kutua na kuruka Juni mwaka huu.
Profesa Mbarawa, amesema ujenzi huo, hadi sasa umefikia asilimia 75.9, ukihusisha kazi mbalimbali, ikiwemo barabara ya kuruka na kutua ndege. Kazi hiyo imefikia asilimia 99 na jengo la abiria, limefikia asilimia 66.
Waziri Mbarawa alisema hayo jijini Dodoma, alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa uwanja huo.
Alisema serikali imetoa fedha kwa wakati, hivyo hakuna sababu kazi hiyo ichelewe kukamilika.
“Nisisitize, mkandarasi kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), hakikisheni uwanja wa ndege unakamilika kwa wakati.
”Tunataka ifikapo Mei, mwaka huu, uwanja wa ndege uanze kutumika kwa sababu, kilichopo kimezidiwa. Hapa tunatarajia ndege za aina mbalimbali zitue,” alisema.
Katika hatua nyingine, Profesa Mbarawa, alisema mkandarasi azingatie bidhaa zinazonunuliwa, ziendane na fedha inayotolewa, wakizingatia usalama wa abiria, kwani ndiyo kipaumbele cha kwanza.
Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS mkoani hapa, Mhandisi Zuhura Amani, alisema wanaendelea na ujenzi, likiwemo jengo la abiria ambapo umefikia asilimia 66 na litakuwa na uwezo wa kuhudumia watu milioni 1.5 kwa mwaka.
Alisema wanaendelea na ujenzi wa mnara wa kuongozea ndege wenye urefu wa meta 56.2, usimikaji wa vifaa na mifumo ya kuongozea ndege, ujenzi wa jengo la zimamoto lenye uwezo, ujenzi wa majengo ya kufua umeme na ujenzi wa jengo la hali ya hewa.
“Kazi zote za ujenzi zinaendelea vizuri na mkandarasi yuko kazini, tunatarajia hadi kufikia Mei, mwaka huu, ziwe zimemalizika, ndege zianze kutua na kuruka kama alivyoagiza Waziri Profesa Mbarawa yakiwa ni maelekezo ya serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan,”alisema.
Mhandisi Zuhura, alisema serikali imetumia sh. bilioni 15.2 kulipa fidia kwa wananchi ambao walipisha mradi huo.
Alisema eneo la kuondoa nyumba na mali katika eneo la kiwanja, tayari limekamilika na wananchi wamelipwa fidia kwa asilimia 100.
“Wananchi ambao mali zao zimeathiriwa na mradi, tayari wamelipwa fidia na serikali, shilingi bilioni 15.2 zimetumika kulipa wananchi 1,919 kwa asilimia 100,”alisema
WANANCHI WAELEZA
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wananchi wanaozunguka mradi huo, waliipongeza serikali kwa kuendelea kutoa fedha kukamilisha mradi huo na wananufaika na fursa mbalimbali.
Mkazi wa Msalato, Michael Mwadu, alisema tangu mradi huo uanze kutekelezwa, wamekuwa wakinufaika na fursa mbalimbali, ikiwemo ajira.
Alisema wengine walijiajiri kwa kupika vyakula kwa wafanyakazi, kufanya kazi za vibarua na ajira za moja kwa moja.
“Kwa kweli mradi huu, umekuwa na manufaa kwetu tangu ulipoanzishwa kwa sababu, tumejipatia ajira na wengine wamelipwa fidia, hivyo kupata kipato ambacho kimebadili maisha kwa kiasi kikubwa,”alisema.




