Na SUPERIUS ERNEST
KATIBU wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenani Kihongosi, ameagiza kuchukuliwa hatua Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manyoni, kufuatia malalamiko ya wananchi.
Kihongosi alimwagiza Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, Dk. James Bwire, kumchukulia hatua kufuatia malalamiko ya wananchi waliodai kutozwa gharama za matibabu nje ya utaratibu.
Kihongosi alitoa maagizo hayo katika mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero za wananchi wa Itigi Wilaya ya Manyoni.
“Mfawidhi analalamikiwa sana, DMO hili liko ndani ya uwezo wako. Uwezo wa kumwondoa unao angalia kupitia utaratibu wako wa kazi, ulifanyie kazi kabla ya Januari 22 sijaondoka nipate ufafanuzi wa hatua ulizochukua, haiwezekani watu wanatakiwa kupata huduma wanatozwa fedha nje ya utaratibu hii haikubaliki,” alisema.
Katika hatua nyingine, Kihongosi alisisitiza watumishi wa umma kutekeleza wajibu kwa kutoa huduma bora kwa wananchi.
“Nafasi hizo mliziomba wenyewe, lazima mziheshimu muwatumikie wananchi kwa heshima na utiifu
“Vitendo vya watumishi kutowahudumia vyema wananchi, ndivyo vinachonganisha viongozi wa Serikali, Chama na wananchi,” alisema Kihongosi.
Akikagua Chuo Cha Veta Wilaya ya Manyoni ambacho kinaendelea na ujenzi, Kihongosi alimwagiza Mkuu wa Mkoa Halima Dendego, kutenga muda wa kuzungumza na wananchi na kutatua changamoto zao.




