Na NASRA KITANA
KOCHA wa Yanga, Mreno Pedro Goncalves, amesema anafurahia kuona wachezaji wake wakielewa staili ya uchezaji anayoifundisha katika timu hatua ambayo itakuwa chachu kwa wachezaji wapya kuingia katika mfumo wake.
Pedro alitoa kauli hiyo baada ya Yanga kutandaza soka safi na kuibuka na ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Mashujaa katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Uwanja wa KMC, Dar es Salaam.
Katika mtanange huo, mabao ya Yanga yalifungwa na Duke Abuya, Pacome Zouzoua, Prince Dube, na Mudathir Yahya, Mohamed Damaro na Laurindo Aurelio ‘Depu’ kila mmoja akiweka kimiani bao moja.
Pedro alisema ana furaha kuona kikosi chake kikianza kufuata anachokifundisha mazoezini hasa mbinu za kiufundi.
“Ninafurahia kuona wachezaji wangu wameanza kuelewa kile ambacho ninakihitaji, hivyo itakuwa rahisi kwao na wachezaji wapya katika mfumo moja kwa moja,” alisema.
Katika dirisha dogo, Yanga imemsajili Damaro, Okello, Depu na kipa Hussein Masalanga kuimarisha kikosi kwa mechi tofauti ikiwemo katika Ligi Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika
(CAFCL).




