Na VICTOR MKUMBO
MAGWIJI wa soka nchini Boniface Pawasa na Mtemi Ramadhan wameyataka mabenchi ya ufundi ya Simba na Yanga kuhakikisha wanawasoma mapema wapinzani wao kuhakikisha wanapata matokeo mazuri ya ugenini katika mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL).
Yanga inatarajia kesho kucheza na Al Ahly ya Misri katika mchezo wa hatua ya makundi utakaopigwa Uwanja wa Al Salam jijini Cairo huku Simba ikipepetana na Esperance de Tunis, utakaochezwa keshokutwa Uwanja wa Stade Olympique Mammadi nchini Tunisia, mechi zote zitapigwa kuanzia saa 1:00 jioni.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wakongwe hao walisema Simba na Yanga zina nafasi ya kufanya vyema katika mechi za ugenini kama kila benchi la ufundi la timu hizo zitazingatia majukumu yao ipasavyo ikiwemo kuwasoma wapinzani.
Mchezaji wa zamani wa Simba, Pawasa alisema Simba bado ina nafasi ya kufanya vyema katika mechi zilizobaki na kurudisha imani iliyotoweka kwa mashabiki.
Alisema benchi la ufundi la Simba linatakiwa kuwasoma wapinzani mapema na kutumia mbinu mbadala kuhakikisha wanapata ushindi katika mchezo huo na kurejesha imani kwa mashabiki wake.
“Benchi la ufundi la Simba linatakiwa kuhakikisha linawasoma wapinzani mapema na kujipanga kutumia mbinu mbadala ili kupata ushindi ugenini.
“Bado Simba ina nafasi ya kufanya vyema kwani hata misimu iliyopita tuliona timu ikipata ushindi ugenini na kufika mbali zaidi,” alisema Pawasa.
Pawasa alisema kitendo cha kuingia na kutoka ya makocha wa Simba imefanya kuishusha kiwango timu hiyo.
“Ndani ya kipindi kifupi Simba imefanya mabadiliko ya makocha kitu ambacho kinawachanganya wachezaji kwani kila mmoja amekuwa akija na falsafa zake,”alisema.
Alisema kila kocha aliyekuja Simba amekuwa na programu na falsafa zake hivyo kuwafanya wachezaji kushinda kutambua wafuate mbinu za nani wanapokuwa uwanjani.
“Kubadili makocha zaidi ya mmoja kwa kipindi kifupi, kimewachanganya wachezaji, hivyo uongozi unatakiwa kutumia mbinu mbadala kuirudisha timu hiyo katika mstari sahihi,” alisema Pawasa.
Kwa upande wake, kiungo wa zamani wa Simba, Mtemi alisema Simba bado ina kazi ya kufanya kuhakikisha inapata matokeo mazuri katika mchezo unaofuata tofauti na Yanga.
Alisema Yanga ina timu nzuri na inaweza kwenda kutoa ushindani zaidi katika mchezo huo wa ugenini.
Alisema kwa Simba mechi inayofuata itakuwa ngumu kwani wakifungwa itakuwa wameondoa matumaini ya kusonga mbele tofauti na Yanga.
Mtemi aliongeza kwa upande wa Simba wanatakiwa kufanya mazoezi ya nguvu kuhakikisha wanawakabili wapinzani wao na kupata ushindi.
“Timu ya Yanga ina nafasi nzuri kwani ina timu yenye wachezaji walio na muunganiko mzuri hivi sasa tofauti na Simba.
“Viongozi wa Simba wanatakiwa kujitathmini na kuangalia wapi walipokosea na kurekebisha mapema ili kuhakikisha wachezaji wanapambana na kupata ushindi katika mchezo huo,” alisema Mtemi.
Katika msimamo wa kundi D, Petro Atletico inaongoza kwa pointi nne sawa na Stade Malien zikitofautiana mabao ya kufunga, nafasi ya tatu inashikiliwa na Esperance de Tunis kwa pointi mbili huku Simba ikiburuza mkia bila pointi.
Kwa upande wa msimamo wa kundi B, Al Ahly ipo kileleni kwa pointi nne sawa na Yanga, zikitofautiana mabao ya kufunga, AS Far ipo nafasi ya tatu kwa pointi moja huku JS Kabylie ikiburuza mkia kwa alama yake moja.




