NA MWANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, anatarajia kuwaongoza Watanzania katika shughuli ya upandaji miti itakayofanyika Januari 27 mwaka huu, maeneo ya Bungi Kilimo na Kizimkazi, Zanzibar ikiwa sehemu ya kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa.
Shughuli hiyo yenye kaulimbiu “Uzalendo ni Kutunza Mazingira, Shiriki Kupanda Miti” linaakisi dhamira ya Rais Dk. Samia katika kuendeleza ajenda ya Taifa ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira, ikiwemo upandaji miti, ulinzi vyanzo vya maji, kuimarisha uoto wa asili na kuchangia kwa vitendo juhudi za kukabiliana dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo ya habari na Mkurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari Machumu, ilisema shughuli hiyo ni ishara ya uwajibikaji wa pamoja na inatoa fursa kwa kila mmoja, kwa nafasi yake na mahali alipo, kushiriki kulinda na kuenzi mazingira kwa manufaa ya sasa na kizazi kijacho.
“Mheshimiwa Rais anatoa wito kwa Watanzania kuendelea kujenga utamaduni wa kulinda na kuhifadhi mazingira kwa hiyari, wakitambua kuwa ulinzi wa mazingira ni msingi wa uhai, maendeleo na usalama wa Taifa,” alisisitiza.
Pia, ilisema Rais Dk. Samia aliwahimiza wananchi, taasisi na wadau wa mazingira kushiriki kuendeleza ajenda ya uhifadhi wa mazingira, ikiwemo kupanda angalau mti mmoja nyumbani, shuleni, kazini au katika maeneo ya jamii.




