Na MWANDISHI WETU
WAKATI ikichuana na Al Ahly leo, Yanga inapaswa kuwa makini na kuongeza ubora wa hali ya juu, kuhakikisha inavunja mwiko wa rekodi ya wapinzani wao.
Yanga itachuana na Al Ahly leo saa 1:00 usiku katika mechi ya tatu ya kundi B Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) katika dimba la Borg El Arab huko Alexandria, umbali wa kilometa 5,668 kutoka uwanja wa Cairo ulipo.
Uwanja huo una uwezo wa kuingiza mashabiki 86,000 waliokaa na una paa moja tu lililofunikwa sehemu ya kukaa viongozi na wageni maalumu.
Katika mtanange huo, Yanga ikiwa na rekodi ya kushinda mechi moja kati ya tatu ilizocheza ugenini itachuana na Al Ahly iliyoonyesha ubabe mara zote ilizokuwa nyumbani msimu huu.
Yanga ilishinda 3-0 ugenini ilipocheza na Wiliete ya Angola katika hatua ya awali ya michuano hiyo huku ikitoka suluhu dhidi ya JS Kabylie katika makundi na kufungwa bao 1-0 kutoka kwa Silver Strikers ya Malawi katika hatua ya pili.
Al Ahly imeshinda bao 1-0 dhidi ya Aigle Noir ya Burundi katika hatua ya pili kabla ya kushinda mabao 4-1 dhidi ya JS Kabylie ya Algeria katika hatua ya makundi.
Katika kundi B, Yanga ipo nafasi ya pili ikiwa na alama nne sawa na kinara Al Ahly zikitofautiana mabao ya kufunga na kufungwa wakati AS Far Rabat ya Morocco na JS Kabylie zikifuatia kwa alama moja kila moja.
Akizungumzia mechi hiyo, Kocha wa Yanga, Mreno Pedro Goncalves, alikiri ubora wa Al Ahly lakini amesema timu yao ipo imara kuwania pointi tatu.
“Tunakwenda kusaka pointi tatu, natumai tutazipata, wachezaji wetu hawana presha kwa sababu wamecheza mechi nyingi kubwa. Al Ahly ni timu nzuri na hatari.
Lakini tumefanya kazi ya kuiangalia na kufahamu jinsi gani tutakwenda kucheza nao katika mechi hii.” alisema.
KAZI IPO HAPA
Kuelekea mpambano huo wa leo, macho ya mashabiki wa soka yatakuwa kuona ubora wa washambuliaji wa Yanga wakiongozwa na Prince Dube, Laurindo Aurelio ‘Depu’ na Emmanuel Mwanengo ambao wanatarajiwa kuipa Yanga nguvu ya kutafuta mabao muhimu ugenini.
Nyota hao watashirikiana na wachezaji wengine kama Pacome Zouzoua, Allan Okello, Mudathir Yahya, Mohamed Damaro na Maxi Nzengeli.
Wachezaji hao watakuwa na kazi ya kuhakikisha wanamfunga kipa wa Al Ahly, El Shenawy na kurudi nchini wakiwa wamechukua pointi tatu.
MSHAMBULIAJI BALAA AL AHLY
Katika mtanange huo, safu ya ulinzi ya Yanga itapaswa kumchunga kwa ukaribu mshambuliaji Mahmoud Hassan maarufu Trezeguet ambaye amekuwa na kiwango bora katika michuano hiyo msimu huu.
Trezeguet, raia wa Misri mwenye umri wa miaka 31, ndiye kinara wa kupachika mabao katika Ligi ya Mabingwa msimu huu, akiwa amepachika mabao matatu katika mechi mbili.
Nyota huyo alifunga mabao mawili dhidi ya JS Kabylie kabla ya kupachika bao moja dhidi ya AS FAR.
Safu ya ulinzi ya Yanga inaundwa na wachezaji mahiri wakiwemo Mohamed Hussein, Ibrahim Hamad, Dickson Job, Bakari Mwamnyeto na Israel Mwenda.
Lakini Al Ahly ina wachezaji wengine hatari wakiwemo Shobeir, Seha, Ben Romdhane, Shoukry, Attia, El Shahat, Bencharki, Taher na Koka.
DAKTARI WA YANGA AFUNGUKA
Daktari wa Yanga, Moses Etutu alisema wamejipanga vizuri kuhakikisha wachezaji wa timu hiyo hawapati athari za kuwepo hali ya baridi nchini humo.
“Tunatengeneza mazingira ya kuhakikisha wachezaji wote wanakuwa vuzri na hali ya Misri ni baridi mno, kwa maana hiyo kuna mabadiliko ya kimwili, kwa mmtu anayetoka kanda yetu ya joto kunakuwa na hali tofauti, tunajitahidi kuwawezesha wachezaji kuzoea na ndio maana wanafanya mazoezi wakiwa na makoti ili kutunza joto na wazoee hali ya baridi,”alisema Daktari huyo.
KUMBUKUMBU MBAYA YA UWANJA
Yanga itashuka Uwanja wa Borg El Arab ikiwa na kumbukumbu mbaya kufuatia kufungwa 2-1 katika mchezo uliochezwa mwaka 2016.
Mabao ya Al Ahly, yalifungwa na Hossam Ghally Abdallah El Said huku Donald Ngoma akifunga bao kwa upande wa Yanga baada ya kupewa pasi na
Juma Abdul.




