RABAT, Morocco
MFALME wa Morocco, Mohammed VI amesema undugu wa Afrika kupitia michezo utaendelea japokuwa taswira yake ilichafuliwa na baadhi ya matukio yaliyotokea wakati wa fainali za michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2025), zilizofanyika nchini Morocco.
Fainali hizo zilimalizika Januari 18, mwaka huu kwa kuzikutanisha Morocco dhidi ya Senegel ambapo wenyeji walipoteza bao 1-0.
Alisema kuna baadhi ya matukio ambayo yaliichafua taswira ya michuano ikiwemo kundi la mashabiki kuvamia walinzi waliokuwa uwanjani.
Alisema kwa muda mrefu, Senegal imekuwa moja ya washirika wa karibu wa Morocco barani Afrika, ambapo makampuni na benki za Morocco zimepanua uwekezaji katika miaka ya hivi karibuni na kuimarisha masuala la kidiplomasia katika ufalme huo.
Alisema saa chache baada ya kumalizika fainali hizo, mitandao ya kijamii katika nchi hizo ilikuwa katika hali ya mvutano kitu ambacho hakikuwa kizuri.
“Fainali iligubikwa na matukio mbalimbali ambayo mengine yalionekana wazi, hii siyo tabia nzuri.
“Japokuwa fainali zilikuwa na mambo mengi, undugu wa Afrika kupitia michezo utaendelea kuwepo.
“Hakuna kitu kinachoweza kudhoofisha uhusiano wa karibu ulioanzishwa kwa karne nyingi kati ya watu wetu wa Kiafrika, wala ushirikiano wenye manufaa uliojengwa na nchi katika bara zima na kuimarishwa kwa ushirikiano uliopo.
“Mashindano hayo pia yalionyesha maendeleo na mafanikio ya Morocco kupitia mchezo wa soka,” alisema.
Hata hivyo, Shirikisho la Soka Afrika (CAF), limesema linaendelea na uchunguzi wa matukio yote yaliyotokea katika mchezo wa fainali huku Rais wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Gianni Infantino akilaani tabia za wachezaji na benchi la ufundi la Senegal.
(Livescore)




