Na AMINA KASHEBA
TIMU za Azam FC na TRA United zinatarajiwa kuonesha kazi katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaopigwa Uwanja wa Azam Complex,Dar es Salaam.
Mchezo huo umepangwa kuchezwa saa 3:00 usiku ambapo Azam watakuwa nyumbani kuwakaribisha TRA United.
Akizungumza Dar es Salaam, Kocha Msaidizi wa Azam, Addis Worku alisema hawakuwa na muda wa kutosha kujiandaa baada ya mechi yao ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAFCC), lakini wapo tayari kwa mchezo wa leo dhidi ya TRA United.
“Wachezaji wamejipanga vizuri kuhakikisha wanafanya vizuri, wanatambua mchezo utakuwa mgumu kwa sababu TRA United wana timu nzuri,” alisema.
Kocha huyo alifafanua kuwa ana imani watafanya vizuri kutokana na uzoefu wa kikosi chake.
“Wachezaji wetu wana uzoefu wa uwanja wetu, hivyo tuna imani watafanya vizuri kwa sababu wapinzani mara nyingi wamekuwa wakijilinda,” alisema.
Mwakilishi wa wachezaji wa Azam FC, Nathaniel Chilambo alisema wanajua umuhimu wa mchezo wa leo na watapambana kuhakikisha wanapata pointi tatu katika mechi hiyo mbele ya TRA United.
“Wachezaji wamejipanga kuhakikisha wanafanya vizuri ili kupata pointi tatu,tunawaomba mashabiki wa Azam waje kwa wingi kutupa hamasa,” alisema.
Kocha wa TRA United, Etienne Ndayiragije alisema kikosi kimesafiri salama kutoka mkoani Tabora na wapo sawa wakisubiri kupambana ili kupata matokeo mazuri.
“Tunategemea baraka za Mungu hivi sasa timu inabadilika na tunaendelea kuzoeana na vijana wanaendelea kuwa na nguvu ya kupambana,” alisema Ndayiragile.
Mchezaji wa TRA United, Omari Yusuf alisema Azam FC ni timu kubwa na wao ni wakubwa pia na wanatarajia mchezo mzuri leo.
“Tumejipanga na wachezaji wana morali ya kutosha kuhakikisha tunafanya vizuri na kupata matokeo katika mchezo wa leo,” alisema.




