Na NASRA KITANA
BAADA ya kupata suluhu dhidi ya Singida Black Stars, Kocha wa Azam FC, Florent Ibenge, amesema kilio chake kikubwa hivi sasa ni wachezaji wake kushindwa kutumia vyema nafasi wanazozipata.
Azam FC ililazimishwa suluhu hiyo juzi katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliopigwa Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.
Ibenge amesema sababu kubwa iliyofanya washindwe kupata matokeo mazuri ni wachezaji wake kukosa utulivu eneo la mwisho hiyo kusababisha kushindwa kupata matokeo.
Amesema ana kazi kubwa ya kuhakikisha anawanoa washambuliaji wake watumie vyema nafasi wanazozipata kutimiza malengo.
“Sare tatu mfululizo siyo kitu kizuri ndani ya timu hiyo inasababishwa na wachezaji wangu kukosa utulivu eneo la mwisho, hivyo nina kazi kubwa ya kufanya kuhakikisha wanatumia vyema nafasi wanazozitengeneza,” amesema Ibenge.
Naye Kocha wa Singida Black Stars, Miguel Gamondi amesema kikosi chake hakijacheza vizuri ila anafurahia kupata pointi moja muhimu.
Alisema kuwa kupata pointi moja ugenini ni jambo zuri lakini anaimani kuwa timu yake itaenda kufanya vizuri zaidi katika mechi zinazofuata.




