Na MWANDISHI WETU
SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na Umoja wa Ulaya kufuatia mafanikio ya ziara ya mashauriano ya ngazi ya juu yaliyofanyika Brussels, Ubelgiji yakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo.
Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Waziri Kombo alizungumza na viongozi wakuu wa Umoja wa Ulaya, wakiwemo, Makamu wa Rais wa Tume ya Umoja wa Ulaya na Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya wa Sera ya Mambo ya Nje na Usalama, Mheshimiwa Kaja Kallas, Kamati ya Kisiasa na Usalama ambayo ni jukwaa kuu la ngazi ya mabalozi la Umoja wa Ulaya kwa ajili ya uratibu wa sera za mambo ya nje, usalama na ulinzi; Makamu wa Rais wa Bunge la Ulaya, Mheshimiwa Younous Omarjee pamoja na Kamishna wa Umoja wa Ulaya anayeshughulikia Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa Jozef Síkela.
Ushirikiano huu unaakisi mwelekeo wa diplomasia ya Tanzania yenye kujiamini, inayozingatia maendeleo, maslahi ya taifa, ushirikiano unaolenga matokeo, na ushirikiano wa kimataifa unaotekelezeka.
Akiambatana na Waziri wa Nchi kutoka Ofisi ya Rais, Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri Kombo alifanya mashauriano ya kina na Kaja Kallas yaliyolenga kuimarisha ushirikiano wa vitendo kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya, hususan katika maeneo ya amani na usalama wa kikanda, biashara inayozingatia utawala wa sheria, uwezeshaji wa uwekezaji, pamoja na mifumo thabiti na inayotabirika ya ushirikiano inayosaidia utekelezaji na ufanisi wa miradi.
Ziara hiyo ilijumuisha mashauriano na Kamati ya Kisiasa na Usalama (PSC) katika makao makuu ya taasisi kuu za Umoja wa Ulaya. Kamati hiyo, inayoundwa na Mabalozi wa Nchi Wanachama wote 27 wa Umoja wa Ulaya na kuongozwa na Balozi wa Urais unaohudumu wa Baraza la Umoja wa Ulaya, ndiyo chombo kikuu cha ngazi ya mabalozi kinachounda na kuongoza sera za mambo ya nje, usalama na ulinzi za Umoja huo.







