Na ATHNATH MKIRAMWENI
KATIBU wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kenani Kihongosi, amesisitiza Chama hakitasita kuchukua hatua kali dhidi ya mtumishi yeyote wa umma atakayehujumu au kuchezea miradi ya maendeleo.
Kauli hiyo aliitoa katika mkutano wa hadhara uliofanyika eneo la Nsimbo, ambapo pia alisikiliza changamoto za wananchi na kuzitatua.
Alisema CCM ina wajibu wa kufuatilia utekelezaji wa miradi iliyomo katika Ilani ya Uchaguzi na kulifananisha jukumu hilo na mwenye duka anayekwenda kukagua biashara yake.
“Sisi ndiyo wenye serikali, lazima tufuatilie miradi yetu. Hatutacheka na yeyote. Mtumishi wa umma atakayejaribu kuchezea miradi ya wananchi tutamchukulia hatua,” alisema.
Akizungumzia miundombinu ya barabara, Kihongosi alisema Mkoa wa Kigoma umepiga hatua kubwa katika sekta ya miundombinu na kuutaja ujenzi wa barabara za lami zinazounganisha wilaya ni utekelezaji wa ahadi za CCM.
Alikumbusha zamani safari ya kutoka Dar es Salaam hadi Kigoma kupitia Tabora ilikuwa ya vumbi na usumbufu mkubwa, sasa hali imebadilika kiasi kikubwa.
Kuhusu gridi ya taifa, Kihongosi alisema mwaka 2022 mkoa wa Kigoma, uliunganishwa rasmi katika gridi ya taifa chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, hatua aliyoondoa utegemezi wa majenereta na kupatikana umeme wa uhakika kwa wananchi na wawekezaji.
Aliongeza CCM itaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo kuhakikisha wananchi wanapata thamani ya kodi zao na ahadi zilizotolewa zinatimizwa kwa vitendo.
Hata hivyo, alisema Chama kipo makini katika kusimamia rasilimali na maendeleo ya taifa.




