REHEMA MAIGALA Na IRENE MWASOMOLA
ASKOFU Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Polycarp Kardinali Pengo, amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 82.
Kutokana na msiba wa kiongozi huyo wa kiroho, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, wametuma salamu za rambirambi, wakimwelezea kwamba, alikuwa kiongozi mzalendo.
Pia, wamesema Kardinali Pengo, atakumbukwa kwa mchango mkubwa alioutoa katika kuimarisha imani, maadili na mshikamano wa kitaifa.
Rais Dk. Samia, alisema taifa limepoteza kiongozi aliyetumikia kwa uadilifu, kujitolea na mchango wake katika malezi ya kiroho, kimaadili utaendelea kukumbukwa, kuthaminiwa na kuenziwa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu, Rais Samia anaungana na kanisa, waumini na Watanzania kwa ujumla katika kipindi hiki cha majonzi na anamwomba Mwenyezi Mungu aipumzishe roho ya marehemu mahala pema peponi.
“Rais Dk. Samia anamkumbuka Kardinali Pengo kama kiongozi wa kiroho na mzalendo aliyetoa mchango mkubwa katika kuimarisha imani, maadili, umoja na mshikamano wa kitaifa kupitia uongozi wake wa muda mrefu ndani ya Kanisa Katoliki.
“Rais Samia anaungana na kanisa, waumini na Watanzania wote kwa ujumla katika kipindi hiki cha majonzi na anamwomba Mwenyezi Mungu, aipumzishe roho ya marehemu mahali pema peponi,”ilisema taarifa hiyo.
Pia, Rais Samia alituma salamu za rambirambi kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Thaddeus Ruwai’chi, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), viongozi wa dini na waumini wote walioguswa na msiba huo.
Aidha, kupitia ukurasa wake wa kijamii wa Instagram, aliandika kuwa, marehemu Kardinali Pengo katika kipindi cha utumishi wake, alisimama imara kuhubiri amani, maadili na mshikamano wa kitaifa.
Rais Dk. Samia, alisema Kardinali Pengo alikuwa sauti ya busara katika masuala ya kijamii, kimaadili, akihimiza amani, heshima na utu.
“Mchango wake katika malezi ya kiroho na maendeleo utaendelea kukumbukwa na kuenziwa siku zote. Ninatoa pole kwa Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Wolfgang Pisa, maaskofu, mapadri, watawa, familia, ndugu jamaa, marafiki, waumini wa Kanisa Katoliki na Watanzania kwa msiba huu,”aliandika.
DK. NCHIMBI
Makamu wa Rais Dk. Emmanuel Nchimbi, jana alitembelea Makazi ya Kiaskofu Kurasini jijini Dar es Salaam, kuwasilisha salamu za rambi rambi za Rais Dk. Samia kufutia kifo cha marehemu Askofu Kardinali Pengo.
Akizungumza akiwa katika makazi hayo, Makamu wa Rais Balozi Dk. Nchimbi alisema, Rais Dk. Samia ameguswa na msiba huo na kuahidi kushirikiana bega kwa bega na Kanisa Katoliki katika msiba huo.
Alisema serikali inatambua mchango mkubwa alioutoa Polycarp Kardinali Pengo katika kipindi cha miaka 42 ya utumishi wake na nia ya serikali ni kuona Kardinali Pengo anazikwa kwa heshima zote.
Kwa upande wake, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mhashamu Askofu Yude Thaddeus Ruwa’ich (OFMCap), aliishukuru serikali kwa mchango iliyotoa wakati wa matibabu ya Kardinali Pengo.
Awali kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Dk. Nchimbi alisema Kardinali Pengo aligusa mioyo ya wengi na kulijenga pamoja kanisa na taifa kwa busara, unyenyekevu na imani thabiti.
“Ninaungana na Mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, katika kutoa pole na kuwafariji waumini wa Kanisa Katoliki pamoja na Watanzania wote kufuatia kifo cha Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Mstaafu Polycarp Kardinali Pengo.
“Tunamshukuru Mungu kwa maisha na utumishi wake uliogusa mioyo ya wengi na kulijenga Kanisa pamoja na taifa kwa busara, unyenyekevu na imani thabiti,”alisema.
RAIS MWINYI
Naye Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, alisema marehemu Kardinali Pengo atakumbukwa kwa mchango wake wa kuliongoza Kanisa Katoliki kwa hekima, unyenyekevu pamoja na juhudi zake katika kuimarisha maadili, amani, na mshikamano wa kitaifa.
Taarifa iliyotolewa jana na Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Zanzibar Raqey Mohamed, ilisema Rais Dk. Mwinyi amewaombea faraja na uvumilivu wote walioguswa na msiba huo na kumuombea marehemu apumzike kwa amani.
“Kardinali Pengo atakumbukwa kwa mchango wake wa kuliongoza Kanisa Katoliki kwa hekima, unyenyekevu, pamoja na juhudi zake katika kuimarisha maadili, amani na mshikamano wa kitaifa,”ilisema.
CCM
Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimesema kinatambua mchango mkubwa wa Kardinali Pengo katika kuhudumia Kanisa Katoliki na taifa kwa ujumla.
Kimesema kupitia uongozi wa kiroho, maadili na huduma za kijamii marehemu Kardinali Pengo katika miaka 55 ya Upadri, miaka 43 ya Uaskofu na miaka 28 ya Ukardinali aliweka alama ya uongozi wa unyenyekevu,mshikamano wa kijamii na kujitolea kwa ustawi wa watu.
Taarifa iliyotolewa jana na CCM na kusainiwa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Taifa (NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo, ilisema katika kipindi hiki Chama kinaungana na Kanisa Katoliki, familia, waumini na Watanzania kuomboleza msiba huu.
“Chama kinaungana na kanisa katoliki, familia, waumini na Watanzania wote kwa kuondokewa na kiongozi wetu wa kiroho,”iIisema.
VIONGOZI WA DINI
Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Alex Malasusa, alisema kupitia marehemu Askofu Kardinali Pengo wamejifunza mambo mengi ikiwemo umoja wa madhehebu, kuheshimiana kati ya dini na dini.
Akizungumza na gazeti hili jana Askofu Malasusa alisema marehemu Kardinali Pengo alikuwa mzalendo halisi aliyetamani kuiona Tanzania moja.
Askofu Malasusa alisema marehemu Askofu Kardinali Pengo alikemea maovu kwa uwazi, alijua nafasi yake kama kiongozi wa kiroho, alijenga heshima kwa jamii na alijitahidi kuwa mtu wa upendo wa watu wote.
SHEIKH MRUMA
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), Nuhu Mruma, alisema marehemu Kardinali Pengo, alikuwa kiongozi anayekubali kushauriwa na mwenye ushirikiano mzuri na taasisi nyingine za dini.
Alisema marehemu Kardinali Pengo katika uhai wake, alikuwa kiunganishi kikubwa katika dini na serikali.
ASKOFU MWAMALANGA
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa na Maaskofu na Mashehe, Amani na Maadili Tanzania, Askofu William Mwamalanga, alisema marehemu Askofu Kardinali Pengo atakumbukwa kwa namna alivyoyaleta pamoja madhehebu ya dini zote hatua iliyochochea kudumisha amani.
BALOZI MULAMULA
Naye Mjumbe Maalumu wa Umoja wa Afrika, masuala ya wanawake, amani na usalama, Balozi Liberata Mulamula, alisema anamkumbuka Kardinali Pengo kwa unyenyekevu wake na mchango wake uliojikita katika kudumisha amani.
Alisema marehemu Kardinali Pengo atakumbukwa kwa kwa namna alivyokemea maovu ya rushwa na uchochezi wa migogoro ya kidini.
Pia Balozi Mulamula alisema marehemu Kardinali Pengo alikuwa mtetezi wa amani na mshikamano miongoni mwa Watanzania wa imani zote.
Taarifa iliyotolewa jana na Askofu Ruwa’ichi, ilisema Askofu Pengo alifariki dunia juzi saa 4:00 usiku katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.
“Ninayo masikitiko makubwa kuwatangazieni kwamba leo (juzi) tarehe 19/2/2026 saa 4:00 usiku huu mpendwa baba yetu Mwadhama Polycarp Cardinal Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam ameitwa nyumbani kwa Baba wa Milele, akiwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam,” alisema.
Pia taarifa hiyo ilisema mwili wa marehemu Kardinali Pengo utaagwa Februari 27 katika kanisa la Mtakatifu Yosefu jijini Dar es Salaam na kuzikwa Februari 28 makaburi ya Kituo cha Hija Pugu.
Ratiba iliyotolewa jana na Kanisa Katoliki Jimbo Kuu Dar es Salaam, ilisema waumini na wananchi wataaga mwili wa marehemu Askofu Kardinali Pengo katika Kanisa la Mtakatifu Yosefu kuanzia saa 1 hadi saa 3 asubuhi kabla ya kupelekwa Kituo cha Hija Pugu kwa maziko.
Marehemu Kardinali Pengo alizaliwa Agosti 5 mwaka 1944 katika kijiji cha Mwazye mkoani Rukwa na kupewa daraja la Upadri Juni 20 mwaka 1971.
Vilevile marehemu Kardinali Pengo aliteuliwa kuwa Kardinali mwaka 1998 na Papa Yohane Paulo II.
Pia marehemu Kardinali Pengo alistaafu rasmi Uaskofu katika Jimbo Kuu la Dar es Salaam mwaka 2019 na nafasi yake kuchukuliwa na Askofu Ruwa’ichi.




