Na AMINA KASHEBA
WAKATI Simba ikipiga vyema hesabu zake kuvuna pointi tatu dhidi ya Dodoma Jiji kesho, Yanga imepania kuendeleza kasi ya ushindi katika michezo ya Ligi Kuu Tanzania Bara kutetea taji hilo.
Timu hizo zimetoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti juzi baada ya kila moja kuvuna pointi tatu.
Simba inayonolewa na Steven Barker ilipata ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Tanzania Prisons katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma wakati Yanga ikishinda 1-0 dhidi ya Namungo katika Uwanja wa Majaliwa, Lindi.
Kila moja ikicheza mechi tisa msimu huu, Simba imeibuka na ushindi mara saba, sare moja na kupoteza mechi moja wakati Yanga ikishinda mechi nane na kutoka sare mara moja.
Kesho, Wekundu hao wa Msimbazi watachuana na Dodoma Jiji katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma wakati Yanga ikivaana na JKT Tanzania katika Uwanja wa KMC, Dar es Salaam.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Kocha wa Simba, Barker, alisema hivi sasa wameelekeza nguvu na akili katika mchezo ujao dhidi ya Dodoma Jiji.
Barker alisema ataiandaa vyema timu yake kwa mchezo huo kuendelea kuvuna alama tatu.
“Tumeshamaliza mchezo na Tanzania Prisons, hivi sasa tunajipanga kwa mechi na Dodoma Jiji, tunarudi uwanja wa mazoezi kufanya mazoezi kuhakikisha tunakuwa bora,” alisema.
Barker raia wa Afrika Kusini, alifurahia kikosi chake kuonyesha kiwango bora katika mchezo dhidi ya Tanzania Prisons.
“Ninawapongeza mashabiki kwa kujitokeza uwanjani na kusapoti timu yao kwani ujio wao umewapa nguvu wachezaji kupambana hadi kufanya vizuri na kuondoka na pointi tatu,” alisema.
Naye nyota wa Yanga, Dickson Job, alisema kila mchezaji anajua umuhimu wa kutetea taji hivyo watapambana katika kila mechi kuhakikisha wanatimiza adhma hiyo.
“Sisi kama wachezaji tunaahidi tutapambana katika michezo iliyobaki kwani tunahitaji kutetea ubingwa, kikubwa mashabiki waendelee kutusapoti,” alisema.
Job aliwashukuru mashabiki wa timu hiyo kwa kuendelea kujitokeza kwa wingi uwanjani hatua ambayo imekuwa ikiipa hamasa timu hiyo kufanya vizuri.
Job alidai kuwa, hivi sasa akili na nguvu zao wamezielekeza katika mchezo dhidi ya JKT Tanzania.




