Na SUPERIUS ERNEST
IMETIMIA miaka mitano tangu kufariki dunia kwa aliyekuwa Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, Dk. John Magufuli.
Katika kipindi hicho Watanzania wanaendelea kukumbuka kazi zilizofanywa na kiongozi huyo, ikiwemo misimamo yake ya kutaka Tanzania ijitegemee kiuchumi.
Imekuwa furaha ya Watanzania kuona miradi aliyoianzisha kiongozi huyo, ikiendelezwa na kukamilishwa na mrithi wake Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye aliwahakikishia wananchi kuwa hakuna kitakacho simama licha ya kuondokewa na Dk. Magufuli.
Dk. Samia ametoa kauli hiyo, wakati akiapishwa kushika wadhifa huo, Machi 19, 2021, siku mbili baada ya kifo cha kiongozi huyo, ambapo alisisitiza kwamba ni wakati wa kutazama mbele kwa matumaini na siyo wakati wa mashaka.
Katika kipindi hiki cha miaka mitano Watanzania wameshuhudia Tanzania nzima ikijengwa kwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati na ile ya huduma za jamii, ikiwemo ya sekta za elimu, afya, miundombinu ya barabara, usafirishaji na maji.
Miradi ya kimkakati ambayo Watanzania wanajivunia ni reli ya kisasa (SGR), Bwawa la Umeme la Julius Nyerere lililopo Bonde la Mto rufiji, daraja la Kigongo Busisi.
Hayo yote yanawafanya wananchi kubaki na furaha wakati wakikumbuka miaka mitano ya baada ya kifo cha Dk. Magufuli, kwa sababu ya msingi imara wa maendeleo aliouweka.
Katika kuadhimisha kumbukizi ya kifo cha Dk. Magufuli , Makamu wa Rais Dk. Emmanuel Nchimbi, leo atawaongoza Watanzania na wanachato kwa ujumla, katika kumbukizi ya kiongozi huyo.
Dk. Nchimbi aliwasili Uwanja wa Ndege wa Geita, jana na kupokelewa na viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali wa Mkoa huo, tayari kwa kushiriki ibada maalumu ya kumbukizi ya kifo cha Dk. Magufuli.
Akielezea tukio hilo la kumbukizi, Mbunge wa Viti Maalumu, Jessica Magufuli, ambaye ni mtoto wa Magufuli, alisema katika tukio hilo, wanatarajia kuongozwa na Makamu wa Rais Dk. Nchimbi.
Pia, alieleza kuwa, katika ibada maalumu itakayofanyika nyumbani kwao Chato, kutaudhuriwa na mgeni maalumu ambaye ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ma viongozi mbalimbali wakiwemo wastaafu.
Aliwakaribisha wananchi mbalimbali, kujitokeza kuungana na familia katika matukio yaliyopangwa kufanywa na familia hiyo ikiwa ni sehemu ya kumuenzi kiongozi huyo.
Alitaja baadhi ya matikio hayo ni kushiriki misa takatifu, chakula cha pamoja na mkesha utakao jumuisha wasanii mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya kumkumbuka kiongozi huyo.
“Katika kumenzi siku hiyo, familia hiyo imeandaa matukio mbalimbali, ikiwemo matembelezi yaliyoambatana na kutenda matendo ya huruma,”alisema.
Baadhi ya matendo hayo ni kujitolea damu katika hospitali ya Chato, kununua mashuka na vifaa tiba mbalimbali.
Alipongeza maendeleo yaliyopo katika hospitali hiyo ikiwa ni jitihada kubwa zinazofanywa na Rais Dk. Samia kupitia utekelezaji ilani ya Chama.
“Kupitia jitihada kubwa za serikali ya Rais Dk. Samia imeweka nguvu kubwa kuhakikisha, hospitali za wilaya zinajengwa na kuwekewa vifaa tiba, hii ni hatua kubwa tunapongeza,”alisema.
Alisema wao kama wanachama wa CCM na viongozi wa Chama, wataendelea kutekeleza ahadi zote zilizoahidiwa katika kipindi cha kamepeni, kuhakikisha zinatekelezwa kuondoa changamoto ya wananchi.
Alisema kwa siku za nyuma ilikuwa kila wazazi 100,000 vilikuwa vikitokea vifo 350, ambapo kwa jitihada za serikali vimepungua hadi sasa kufikia vifo 104.
Jessica alieleza kuwa, katika kipindi cha Rais Dk. Samia, kazi kubwa imeendelea kufanyika katika sekta mbalimbali, ambapo na yeye ni mbunge wa viti maalumu, akiwa katika kamati ya TAMISEMI.
Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, alisema katika kipindi cha miaka mitano ya kifo cha Dk. Samia, wameendelea kukumbuka kazi kubwa aliyoifanya kwa Watanzania.
Alisema kuwa, wanamkumbuka kwa umahiri wake wa uongozi na kazi aliyoiacha inaendelezwa na Rais Dk. Samia, ambaye ameendelea kuchochea miradi mbalimbali, ikiwemo ya kimkakati.
Alieleza kuwa wataendelea kumkumbuka kwa mema yake na kumuombea kwa mwenyezi mungu.
Makonda aliyasema hayo juzi, alipomtembelea Mkuu wa Majeshi Mstaafu, Venancy Mabeyo, akimuomba kumwakilisha katika kumbukizi hiyo Chato, kwani yeye atakuwa na majukumu mbalimbali ya wizara kuelekea katika mashindano ya Afcon 2027.
Katika hatua nyingine, Mabeyo, alimshukuru Makonda kwa kumtembelea na kuahidi kufika Chato kwa ajili ya kumbukizi hiyo, kumuenzi kiongozi huyo.
Alisema anaendelea kumkumbuka kiongozi huyo kwa kazi kubwa aliyoifanya, huku wakiendelea kumuombea mapumziko mema.
Serikali imeendelea kutekeleza azima yake ya kumuenzi hayati Dk. Magufuli, kwa kuungana na familia yake na Watanzania kila Machi 17, ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wake katika uongozi wa nchi.




