Na MWANDISHI WETU
MAMLAKA ya Hali ya Hewa nchini (TMA), imetangaza kunyesha mvua kubwa siku tano mfululizo katika mikoa nane nchini, huku ikitoa angalizo kwa wananchi kuchukua tahadhari kuepuka athari.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na mamlaka hiyo, mvua inatarajiwa kunyesha kesho katika mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Morogoro, Lindi, Mtwara na Pwani huku ikijumisha visiwa vya Mafia na Unguja na Pemba.
Taarifa hiyo ilitaja athari zinazoweza kujitokeza ni baadhi ya makazi kuzungukwa na maji, hivyo kila mwananchi anatakiwa kuchukua tahadhari.
“Kuna uwezekano wa kutokea athari kwa sababu ya mvua hiyo,” ilieleza taarifa ya TMA.
Ilibainisha kuna haja ya kuchukua tahadhari ya mvua hiyo leo, hususan mikoa ya Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Tanga, Dar es Salaam, Morogoro, Lindi, Mtwara na Pwani ikijumuisha visiwa vya Mafia pamoja na Unguja na Pemba.




