Na Celina Mathew
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema Tanzania ina Rais jasiri, shupavu na mchapakazi, na kuwataka Watanzania kumuombea na kumtia moyo ili aendelee kuwaletea maendeleo.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Kihongosi, ameitoa kauli hiyo akizungumza na wanachama na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Runazi, Kata ya Kasharunga, Wilaya ya Muleba mkoani Kagera.
Kihongosi amesema sifa hizo ndizo zinazoonyesha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anaendelea kufanya kazi kwa moyo wa dhati, licha ya changamoto na ukosoaji kutoka kwa baadhi ya watu.
“Angekuwa mtu mwingine, lazima moto ungewaka. Lakini kwa kuwa ana upendo na ni mvumilivu, tunamuombea na kumtia moyo ili aendelee kutuletea maendeleo,” amesema Kihongosi.
Aidha, amesisitiza kuwa Watanzania wote wanapaswa kushirikiana kumuunga mkono Rais Dk. Samia ili miradi ya maendeleo iendelee kufanikishwa kwa manufaa ya wananchi.




