Na WAANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwaongoza Watanzania, kutoa heshima za mwisho kwa aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Utaratibu) William Lukuvi, ambaye pia alikuwa Mbunge wa Jimbo la Ismani mkoani Iringa katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa, iliyotolewa juzi, Dodoma na Ofisa Mwandamizi wa Bunge, anayeshughulikia Habari, Mawasiliano, Elimu kwa Umma, Patson Sobha.
Pia, alisema Rais Dk. Samia, anatarajiwa kuwaongoza Watanzania, katika mazishi ya Lukuvi, yatakayofanyika Idodi, Iringa vijijini Machi 31, mwaka huu, baada ya kuagwa na wananchi wa Iringa Mjini, eneo la Gangilonga Machi 29.
Ikubukwe kuwa jana ilikuwa ni nafasi ya wabunge, viongozi mbalimbali na wananchi wa mkoa wa Dodoma kuaga mwili wa kiongozi huyo, ambapo waliongozwa na Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba.
DK. EMMANUEL NCHIMBI
Makamu wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, alisema Lukuvi atakumbukwa daima, kwani alikuwa kiongozi mchapakazi na mzalendo, aliyetoa mchango mkubwa kwa taifa, jimbo lake, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Umoja wa Vijana (UVCCM).
Alisema anaungana na Rais Dk. Samia kuomboleza kifo cha Lukuvi na anatoa salamu za pole kwa Spika wa Bunge, Mussa Azzan Zungu, wabunge, familia ya marehemu, ndugu, jamaa, marafiki na wananchi wote wa Jimbo la Isimani.
DK. MWINYI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, alisema atamkumbuka Lukuvi kwa mchango wake mkubwa na kwamba kifo chake ni pigo kubwa kwa taifa.
Alisema wamempoteza kiongozi mzoefu, mzalendo na aliyejitolea kwa dhati kutumikia taifa kwa muda mrefu katika nyadhifa mbalimbali za uongozi.
Rais Dk. Mwinyi alitoa salamu za pole kwa Rais Dk. Samia, Spika wa Bunge, Azzan Zungu, familia ya marehemu, ndugu, jamaa, marafiki, wananchi wa Jimbo la Isimani na Watanzania, kufuatia msiba huo, huku akisema yupo na familia ya marehemu na serikali kwa ujumla katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza kifo cha kiongozi huyo.
WAZIRI MKUU DK. NCHEMBA
Akiwaongoza wananchi wa Dodoma na viongozi mbalimbali, Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba alisema marehemu Lukuvi ataendelea kukumbukwa kwa weledi wake mkubwa, ushawishi wa kazi na uratibu wake na mshauri mzuri.
Alieleza kuwa Lukuvi alikuwa mlezi, mwalimu na mshauri wa kila mbunge na waziri akiongozwa na nidhamu binafsi ya kazi, akijituma hali iliyo sababisha viongozi kumwamini na kumpa majukumu mbalimbali.
Mwigulu alitoa pole kwa familia na ndugu wote, huku akisema serikali itaendelea kushirikiana nao wakati wote, wakiendelea kukumbuka busara zake na ukomavu wake katika uongozi.
DK. MPANGO
Makamu wa Rais Mstaafu Dk. Philip Mpango, alisema sifa za Lukuvi ni nyingi, kwani alikuwa hazina kubwa, alitumika zaidi kuwafunda viongozi wa serikali kwa umahili mkubwa.
Alisema anakumbuka walivyoshirikiana vyema katika awamu ya tano yeye akiwa Waziri wa Fedha, ambapo kiongozi Lukuvi alimpongeza kwa uimara mkubwa katika uongozi wake, jambo lililomtia moyo zaidi katika utendaji wake.
Alitoa pole kwa ndugu na familia, akiwataka kujipa moyo na kuendelea kumwamini Mwenyezi Mungu, kuachana na upotoshaji wa mitandaoni unaotokana na matumizi mabaya ya mitandao.
Kwa upande wake, Spika mstaafu wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, alisema kifo cha kiongozi huyo kimeacha pengo kubwa kwa serikali, huku akitoa pole kwa Rais Dk. Samia, spika wa bunge na wananchi wa Isimani.
Alisema namna njema ya kumuenzi kiongozi huyo ni kuendelea kuyaishi mema yote aliyoyatekeleza kipindi cha uhai wake, huku akisema mchango wake utakumbukwa daima.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye ulemavu), Ummy Nderiananga, alisema atamkumbuka Lukuvi kwa nasaha zake walipokuwa wakizungumza mara kwa mara.
Alisema mara kwa mara kiongozi huyo, alisisitiza utumishi wenye uzalendo usio na ubadhilifu wala uzembe, alitaka bidii ya kazi.
JAJI MKUU
Jaji Mkuu, George Masaju, alisema taifa limepoteza kiongozi hodari aliyekuwa mdau wa kufuata sharia na kupenda haki.
Alisema alitoa mchango mkubwa kwa serikali, alikuwa mzalendo, mtulivu na mwenye busara kubwa ambaye alikuwa kioo kwa viongozi wengine.
VYAMA VYA SIASA
Wanasiasa kutoka vyama mbalimbali mkoani Iringa ambao waliwahi kufanya kazi na Lukuvi walielezea masikitiko yao kufuatia kifo chake wakimtaja ni kiongozi imara aliyetoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.
DAUDI MASASI
Kamishna wa ADC kanda ya Iringa alisema, Lukuvi atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika siasa za mageuzi na uwezo wake wa kushirikiana na watu wenye itikadi tofauti kwa lengo la kuleta maendeleo.
PETER MSINGWA
Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),Peter Msingwa alisema kifo cha Lukuvi ni pingo kubwa siyo kwa wananchi wa Iringa bali ni cha taifa kwa jumla.
Alisema Lukuvi alikuwa kiongozi jasiri mwenye msimamo thabiti na aliyejitolea kuwatumikia wananchi wake kwa moyo mmoja.
BALOZI LIBERATA MULAMULA
Waziri mstaafu wa Wizara ya Mambo ya nje,Ushirikiano wa Afrika Mashariki,Balozi lIBERATA Mulamula alisema,Lukuvi ndiye aliyekuwa ‘Chief Whip’ bungeni alikuwa anawaongoza na kuwaelekeza wabunge.
“Siwezi kusema nilifanya naye kazi maana alikuwa ni kiongozi wetu muandanizi.Binafsi nilijifunza mambo mengi kutoka kwake nikiwa bungeni alikuwa kama mwalimu wangu, kwa kweli kifo chake ni pigo kubwa kitaifa ameacha pengo kubwa katika serikali na bungeni,”alisema.
PROFESA KABUDI
Waziri wa nchi,Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu),Paramagamba Kabudi alisema alisema Lukuvi atakumbukwa kwa kufanya kazi zake kwa kujituma bila kuchoka na kwa ushirikiano mkubwa.
“Tutamkumbuka daima kwa mengi ucheshi wake,utanashati wake,uzoefu wake wa miaka mingi na busara zake.
HAMADI CHANDE
Naibu bWaziri wa Maliasili na Utalii,Hamadi Chande alisema,Lukuvi alikuwa ni mtu wa aina yake mpole na mwenye moyo wa kusaidia wengine hasa wahitaji.
Alisema alikuwa ni mzoefu bungeni na alipokea wange wengi na kuwafundisha kazi, wengi waliopita katika mikono yake wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa.
“Lukuvi alikuwa ni muumini wa kupenda watu wote na kujali bila ya kujali unatoka mkoa gani na kufanikiwa kutuunganisha pamoja hata alipokuwa Waziri wa Ardhi pia aliwasikiliza watu wote bila ya kubagua,”alisema.
MAWAZIRI WAZUNGUMZA
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, alisema, Lukuvi alikuwa kiongozi mchapakazi na mwenye maono ya kizalendo kwa taifa lake.
Alisema mara nyingi alikuwa anafanya kazi zake kwa kufuata utaratibu uliopo ikiwemo sera.
“Tumempoteza kiongozi shujaa, mpenda watu, mzalendo, mtiifu na aliyekuwa anapenda maendeleo ya nchi yake,”alisema Kairuki.
MOHAMED MCHENGERWA
Waziri wa Afya, Mohamed Mchengerwa, alisema amejifunza mambo mengi kutoka kwa Lukuvi ikiwemo namna alivyoishi karibu na wananchi wake.
JUDITH KAPINGA
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga, alisema taifa limepoteza kiongozi muhimu aliyependa kazi yake na alikuwa mzalendo katika kuwatumikia wananchi.
“Mezani kwa Lukuvi hakuna jambo lililokuwa linalala, ukimpelekea jambo lako alikuwa analichukua kama lake na kulisukuma hadi mwisho,” alisema Judith.
JUMAA AWESO
Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, alisema Lukuvi alikuwa mtu anayependa kujituma bila kushurutishwa ikiwemo kufuata sheria na kanuni katika uongozi wake.
Alisema alipenda kuona matokeo katika kazi anazofanya na kusimamia haki katika nyanja mbalimbali.
“Alipokuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, alitatua kero nyingi za wananchi. Hata bungeni alikuwa akifanya kazi kwa uadilifu mkubwa, tumekuwa tukimwona kama mwalimu na mfano wa kuigwa,” alisema Aweso.
DAVID KIHENZILE
Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, alisema wamepokea kwa masikitiko taarifa za msiba huo uliotokea ghafla.
Alisema Lukuvi alikuwa kiongozi aliyetoa mchango mkubwa nchini, mwadilifu, mchapakazi na mwalimu wa viongozi vijana wakati wote.
“Amekaa bungeni kwa muda wa miaka 30; hii inadhihirisha wananchi wake walimpenda na kumwamini. Kuondoka kwake kumeacha pengo kubwa, kwani amehudumu serikalini muda mrefu na kwa weledi,”alisema.
Kihenzile alisema Iringa na taifa limepata pigo kutokana na kifo cha kiongozi huyo aliyekuwa na uzoefu wa miaka mingi serikalini.
WABUNGE WAELEZA
Baadhi ya wabunge kutoka mkoani Iringa, wamesema kifo cha Lukuvi ni pigo kubwa kwa mkoa huo kutokana na mchango wake mkubwa wa maendeleo.
RITTA KABATI
Mwenyekiti wa Wabunge Mkoa wa Iringa, Ritta Kabati, alisema moja ya jambo kubwa analolikumbuka kutoka kwa Lukuvi ni namna alivyokuwa anapenda umoja na maendeleo kupitia ujenzi wa miradi ya maendeleo.
MZEE KIMITI
Mwanasiasa mkongwe, Paul Kimiti, alisema nchi imepoteza kiongozi imara aliyekuwa akijituma katika kazi za maendeleo ya nchi.
Alisema alimfahamu Lukuvi mwaka 1991 alipokuwa Naibu Waziri wa Kazi na Maendeleo ya Vijana.
Hata hivyo, Kimiti alieleza sababu ya Lukuvi kudumu katika uongozi ilitokana na ujasiri, mvumilivu na uchapa kazi hodari aliokuwa nao katika majukumu yake.
“Ndiyo maana wananchi wake wa Jimbo la Isimani kila uchaguzi walikuwa hawana wa kumchagua dhidi ya Lukuvi kwa sababu alikuwa ni kiongozi anayependa maendeleo,” alisema.
Kimiti alisema uchapakazi na uzalendo wake, vilimvutia Rais Dk. Samia kumchagua katika nafasi za uongozi.
“Rais Dk. Samia na viongozi wengine wa nchi hawakuwahi kumwacha Lukuvi katika nafasi za uongozi kwa sababu ya usikivu na uhodari katika kazi zake,” alisema Kimiti.
Alisema hawezi kumsahau Lukuvi kwa sababu alikuwa mikononi mwake ambapo wakati wote alionesha shauku ya kujifunza.
MARY CHATANDA
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Chatanda, alisema anamfahamu Lukuvi kwa muda mrefu tangu akiwa kiongozi wa UVCCM.
Mary alisema Lukuvi alikuwa ni mbunge mwenye msaada mkubwa kwa wananchi wa Jimbo la Isimani.
Alisema ndani ya bunge alikuwa mwalimu wa wabunge wapya kwa sababu alikuwa anapenda kuwaeleza mengi.
“Mara nyingi wabunge wadogo walikuwa wanapenda kumwita Lukuvi mwalimu au seneta, ameacha pengo katika sekta siasa,”alisema.
GEORGE MKUCHIKA
Mwanasiasa mkongwe nchini, George Mkuchika, aliwapa pole wananchi wa Isimani, wabunge na Watanzania kwa kumpoteza mbunge huyo makini.
Mkuchika alimweleza Lukuvi ni mtu aliyejali wananchi wa jimbo hilo.
“Alikuwa anawajali watu wake, kipindi kile ilikuwa haiwezi kupita wiki moja bila ya kwenda jimboni kwake kutatua matatizo ya wananchi wake,” alisema.
CCM IRINGA
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, Daudi Yassin alisema Chama kimepoteza kiongozi mwadilifu, mzalendo, mchapakazi na mpenda maendeleo.
Alisema watamkumbuka kwa mchango wake mkubwa wa kutumikia taifa na wananchi wa Mkoa wa Iringa kupitia jimbo la Isimani.
“CCM inatambua kazi kubwa ambazo alizifanya kwa uzalendo na kujitolea. Tumepoteza kiongozi mwadilifu sana na mpenda maendeleo katika taifa,” aliongeza Yassin.
TAARIFA YA KIFO
Taarifa ya kifo, ilitolewa Machi 24, mwaka huu, kwa umma na kutiwa saini na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Moses Kusiluka, ilisema Lukuvi alifariki dunia katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma, alikokuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa mshtuko wa moyo.
“Rais alitoa pole kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, familia, wananchi wa Jimbo la Isimani, ndugu, jamaa, marafiki na Watanzania wote kwa msiba huo,” ilisema taarifa hiyo.
WASIFU
Lukuvi alizaliwa Agosti 15, mwaka 1955, Kijiji cha Mapogoro, Wilaya ya Iringa Vijijini, Tanganyika, mkoani Iringa.
Alisoma Shule ya Msingi Kitanewa kuanzia mwaka 1962 hadi mwaka 1970. Alipata mafunzo ya awali katika Chuo cha Ualimu Tabora (TTC) na kuhitimu baadaye aliendelea na masomo ya shahada ya uzamili katika sayansi ya siasa kutoka Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT).
SAFARI YA KISIASA
Lukuvi alianza safari ya kisiasa kwa kuchaguliwa Mbunge wa Jimbo la Isimani mwaka 1995, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), nafasi ambayo aliishika hadi kifo chake.
Aidha, alihudumu katika nafasi ya naibu waziri na waziri katika nyadhifa mbalimbali.
Januari 2015 hadi Januari 2022 alikuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Bunge), Novemba 2010 hadi Januari 2015.
Pia, Juni mwaka 2023, Rais Dk. Samia alimteua kuwa Mshauri wa Rais katika Uhusiano wa Kisiasa na Kijamii, ambapo hadi kifo chake alikuwa Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Bunge).
Vilevile, Lukuvi aliwahi kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Mjumbe wa Kamati ya Maadili ya Kamati Kuu CCM, mkuu wa wilaya na baadaye mkuu wa mikoa mbalimbali.
DONDOO ZAIDI
1975-1980 – Mwalimu
1980-1994- Uongozi Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)
1994-1995- Mkuu wa Wilaya Bukoba
1995- Bungeni
1995- 2000- Naibu Waziri wa Vijana na Kazi
2000-2005-Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu)
2006-2010- Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dar es Salaam
2010-2015- Waziri
2015-2022- Waziri wa Ardha, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
2023-Mshauri wa Rais
2024-2026- Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu).




