Na NASRA KITANA
UONGOZI wa klabu ya Simba umepania kuhakikisha wanalipa kisasi katika mchezo dhidi ya Azam FC, baada ya kupoteza mechi mbili mfululizo zilipokutana.
Mchezo wa kwanza Simba dhidi ya Azam FC msimu huu ulichezwa Desemba 7 mwaka jana, Wekundu wa Msimbazi walikubali kichapo cha mabao 2-0 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam.
Pia Simba ilipoteza bao 1-0 dhidi ya Azama, timu hizo zilipokutana kwa mara ya pili katika michuano ya Kombe la Mapinduzi, mechi iliyofanyika Januari 8, mwaka huu.
Timu hizo zinatarajiwa kushuka dimbani Aprili 5, mwaka huu katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, itakayofanyika Uwanja wa Azam Complex, Chamanzi.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally alisema kuwa hawatakubali kuona wanarudia makosa waliyofanya mechi zilizopita, mchezo huo watahakikisha wanalipa kisasi.
Alisema wanajua Azam ni timu bora na wamewafunga katika mechi mbili zilizopita, lakini safari hii hawatakubali kuona wanapoteza.
“Tunajua mchezo utakuwa mgumu na wenye changamoto kubwa lakini hatutakubali kuona tunapoteza kwani tunahitaji ushindi ili kuweza kulipa kisasi,” alisema Ahmed.
Ahmed alisema kuwa hawana hofu na kikosi waliochokuwa nacho kwani Kocha Steve Baker anajua mapungufu ya kikosi, hivyo atafanya marekebisho ili kiweze kuwa bora na cha ushindani zaidi.
Alisema kuwa hawaiogopi Azam, pamoja na kupoteza mara mbili katika michezo yao na hivi sasa watahakikisha wanakwenda kuweka rekodi yao vizuri.
Ahmed alisema kuwa maandalizi kuelekea katika mchezo huo yanaendelea vizuri huku kocha akisubiria wachezaji wengine ambao wapo katika kikosi cha Taifa Stars.
Naye Ofisa Habari wa Azam FC, Thabit Zacharia ‘Zaka za Kazi’ alisema kuwa wanataka kuendeleza historia yao ya kuifunga Simba.
Alisema anajua Simba hawatakubali kupoteza mchezo huo kwani kila mchezaji ana morari ya kutosha kuhakikisha anapambana mwanzo mwisho ili kupata ushindi.
“Tunajua hautakuwa mchezo mwepesi kwetu, tutapambana mwanzo hadi mwisho kuhakikisha tunapata ushindi katika mchezo huo muhimu na kuendeleza historia yetu,” alisema Zaka.
Katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi 31 baada ya kushuka dimbani mara 14 huku Azam FC ikishika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 29 baada ya kushuka dimbani mara 15.




