Na EMMANUEL MOHAMED
UNYWAJI wa chai ya moto kupita kiasi pamoja na uji wa moto umetajwa kuwa miongoni mwa sababu zinazoweza kuongeza hatari ya kupata saratani ya koo.
Akizungumza na UHURUONLINE, Daktari Bingwa wa Saratani kutoka Hospitali ya Ocean Road, Dk. Sadiq Siu, amesema kuwa watu wengi wamezoea kunywa vinywaji vikiwa vya moto kupita kiasi, hali ambayo inaweza kuathiri afya ya koo.
Amesema joto kali linaweza kusababisha mabadiliko katika seli za ndani ya koo, jambo linaloweza kuchochea kuanza kwa saratani.
“Kinachotokea ni kuwa joto hilo husababisha seli za eneo husika kuanza kubadilika. Tukumbuke kuwa viungo vya ndani ya mwili hubadilika kwa haraka endapo vitapata athari,” amesema.
Dk. Sadiq ameongeza kuwa mabadiliko hayo ya seli yanaweza kuathiri utendaji wake wa kawaida na hatimaye kusababisha saratani.
“Tunapozungumzia saratani, tunazungumzia pia tabia hatarishi.
Miongoni mwa tabia hizo ni kunywa vinywaji vya moto kupita kiasi.
Kuna watu hadi chai lazima iwaunguze ndipo wanywe, hii si tabia salama,” amesema.
Aidha, ametaja mambo mengine yanayoongeza hatari ya kupata saratani ya koo kuwa ni matumizi ya tumbaku na ugoro.
Mbali na hilo, amesema ugonjwa huo pia unahusishwa na unywaji wa pombe kupita kiasi, uvutaji wa sigara pamoja na unene uliopitiliza.




