Na AMINA KASHEBA
UONGOZI wa Chama Cha Netiboli Tanzania (CHANETA) umesema una imani na Tume Huru ya Uchunguzi iliyoundwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kuchunguza vurugu zilizotokea Oktoba 29, mwaka jana.
Akizungumza Dar es Salaam, Mwenyekiti wa CHANETA, Stella Mwangomale amesema ana imani tume hiyo chini ya Mwenyekiti wake, Mohammed Chande Othman ambaye ni Jaji Mkuu mstaafu italeta majibu sahihi kutoka na weledi wa viongozi waliomo.
Aidha, Mwenyekiti huyo alisema amani ni kitu muhimu katika nchi kwa sababu inasababisha uchumi unakua kupitia michezo ambapo vijana wanashiriki mashindano mbalimbali ambayo yanawapatia heshima kimataifa na kukuza uchumi wao.
“Nchi ikiwa na amani kila kitu kinakwenda vizuri hivyo kwangu nina imani na tume huru iliyoundwa na Rais Dk. Samia kwa sababu tuliona kipindi cha vurugu shughuli mbalimbali zilisimama zikiwemo za michezo.
“Hakuna mtu yoyote ambaye alijitokeza uwanjani kufanya jambo lolote hiyo, ukweli pale uchumi ulishuka katika michezo, Watanzania wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kulinda amani ya taifa kwani ndiyo tunu muhimu kwetu,” alisema.
Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa nchi ikiwa na amani ni heshima na itaweza kupata uwenyeji wa michuano mbalimbali na hapo uchumi utaweza kukua.




